HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

November 23, 2014

SIKU 16 ZA KUPINGA UKATILI WA KIJINSIA KUANZA NOVEMBA 25

Mratibu wa Shirika la Wanawake katika Maendeleo barani Afrika (WiLDAF), Judith Odunga akifafanua jambo wakati wa akitoa taarifa kuhusu Siku 16 za kupinga Ukatili wa Kijinsia, inayotarajiwa kuanza Novemba 25 hadi Desemba 10 mwaka huu. Kushoto ni Bahati Mandogo kutoka Kampuni ya JBS na Ofisa wa Polisi Dawati la Kijinsia, Christina Onyango.

Na Mwandishi Wetu


ASILIMIA 92 ya wanawake nchini  wametaka mila na utamaduni unaolazimisha mwanamke akeketwe ukomeshwe kwa sababu kitendo hicho ni sawa na ukatili wa kijinsia.


Kauli hiyo imetolewa leo jijini Dar es Salaam na Mratibu wa Shirika la Wanawake katika Maendeleo barani Afrika (WiLDAF), Judith Odunga, wakati alipokuwa akitoa taarifa kuhusu Siku 16 za kupinga Ukatili wa Kijinsia, inayotarajiwa kuanza Novemba 25 hadi Desemba 10.


Alisema hivyo kutokana na utafiti uliofanywa na Idara ya Takwimu (TDHS), mwaka 2010 na kuonesha kuwa asilimia 82 ya wanawake wenye umri kati ya miaka 15 hadi 49 walikeketwa.


“ Ukimya katika masuala ya ukatili wa kijinsia unachangia katika kushamiri kwa vitendo hivi na hakika bado tuna safari ndefu katika kutokomeza ukatili huu wa kijinsia,”alisema Judith.


Alisema jamii haina budi kuongeza nguvu katika mapambano ya kutokomeza vitendo hivyo vya ukatili wa kijinsia ili kuwa na wanawake wenye afya na familia zenye afya kwa ujumla wake.


Akizungumzia maadhimisho hayo, alisema Mashirika ya Haki za binadamu , wadau wa maendeleo na Asasi za Kiraia wanaungana na wadau wengine wa haki za binadamu duniani kupinga vitendo hivyo aktika siku hizo 16.


Judith, alisema katika siku hizo za kupinga ukatili wa kijinsia kutakuwa na shughuli na midahalo mbalimbali ambapo kwa Dar es Salaam yatafanyika katika viwanja vya Karimjee huku mgeni rasmi akitarajiwa kuwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda.


“Mbali na uzinduzi huo utakaofanyika kitaifa Dar es Salaam, maadhimisho haya pia yatafanyika katika kanda mbalimbali.

Judith, alizitaja Kanda hizo kuwa ni Kaskazini, Ziwa, Kati, Kusini na Nyanda za juu Kusini Magharibi.


Aidha, katika siku hizo katika maeneo hayo elimu mbalimbali kupitia midahalo, mikutano na semina, itatolewa na Asasi na mashirika yote katika maeneo husika.                                            

No comments:

Post a Comment

Pages