HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

March 23, 2015

Mtibwa kimenuka tena, Waziri aridhia Wafanyakazi kumgomea Mwekezaji

Na Bryceson Mathias, Mvomero.

MAANDAMANO na Migomo Kwa Kiwanda cha Sukari Mtibwa mkoani Morogoro, imekuwa kama ni maisha yao ya  kila siku, ambapo pia leo wamemgomea Mwekezaji wa Kiwanda hicho, huku Naibu Waziri wa Maji na Mbunge wa Jimbo la Mvomero, Amosi Makala, akidaiwa kuridhia Mgomo huo.

Taarifa za Makala kuridhia Mgomo huo zilitangazwa kwa Wafanyakazi na Wakulima Wadogo wa Miwa Mtibwa na Katibu wa Mbunge huyo, Juma Kombo, kwamba Naibu Waziri Makala, amedai Waendelee kuwa nje ya Lango la Mwekezaji na yeye Makala atapeleka Chakula hapo hapo.

“Nimeagizwa na Mbunge na Naibu Waziri wa Maji Makala kuwa, Wafanyakazi wasitoke na waendelee kuwepo langoni kwa mwekezaji na yeye atatuma Chakula cha kula Wafanyakazi na Wakulima Wadogo wanaodai haki zao, hadi atakapowalipa”, Kombo aliwaambia Wananchi hao.

Hatua za Makala inakuja baada ya siku mbili kabla Katibu wake, Kombo, kufika kwa Meneja wa Kiwanda hicho, Hamad Yahaya, kwa Mazungumzo ya mezani ili awalipe Wakulima na Wafanyakazi hao Mishahara ya Miezi miwili na Wakulima wa Miwa, lakini kama kawaida, hakuwalipa.

Wafanyakazi hao pichani wakiwa kwenye Lango la Mwekezaji wamesema, Wasingependa kusikia Kauli ya Mbunge wao na Naibu Waziri Makala kupitia kwa Katibu wake, bali walitaka wamuone akilala langoni kwa mwekezji na kula chakula hicho kama ilivyokuwa kwa Chama cha Chadema.

Waliongeza kusema,“Tunakubali mateso haya tunayofanyiwa na Mwekezaji kwa kipindi hiki, lakini Mateso haya yatageuka Kilio kwa Chama cha Mapinduzi kwenye Uchaguzi wa mwaka huu kwenye Kura ya Maoni ya Katiba inayopendekezwa na Uchaguzi Mkuu”, alisema Juma Salumu.

Afisa Utumishi na Uendeshaji wa Mtibwa aliyejulikana kwa jina amoja Mazengo, alikuwa hana Maneno ya kueleza kutokana na kuzongwa na Wafanyakazi, ambapo kila alipoulizwa maswali alishindwa kujibu kutokana na kuzingirwa na wafanyakazi wakisema watabaki naye hapo usiku wote hadi walipwe.


aidha Tanzania Daima lilimtafuta Mbunge na Naibu Waziri Makala kwenye simu yake ya kiganjani kuthibitisha kauli yake lakini hakupatikana, ambapo pamoja na kumkosa liliwasiliana na mwandishi wake aliyeko bungeni, Damson Kaijage, ili kupata uthibitisho wa kauli hiyo, ambapo Kaijage aliahidi kumtumia Karatasi kupata majibu lakini hadi tunakwenda mitamboni tulikuwa hatujapata jibu.

No comments:

Post a Comment

Pages