HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

June 27, 2016

MWANAHARAKATI WA UDHALILISHAJI ZANZIBAR AUAWA

Na Mwandishi wetu, Zanzibar

MWANAHARAKATI wa udhalilishaji wanawake na watoto, Zaituni Juma (Mama Mkapa), ameuawa kwa kukatwa mapanga na watu wasiojulikana nyumbani kwake Bambi, Mkoa wa Kusini Unguja.

Bi. Zaituni ambaye alikuwa akifanya kazi bega kwa bega na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake (TAMWA), alifikwa na mauti juzi, Jumamosi, Juni 26, 2016 majira ya jioni,  alipokutwa peke yake  nje ya nyumba yake na kuvamiwa na wahalifu hao na kumpiga hadi kumtoa roho.

 Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kusini Unguja, Juma Saad, alisema watu wasiojuilikana mnamo majira ya jioni siku hiyo wakiwa wamefunika nyuso walimvamia na kumkata mapanga hadi kumuua.

 Alieleza kuwa tayari wanamshikilia mtu mmoja ambaye anafanyiwa mahojiano ili kuthibitisha kama anahusika au la, na kudai kwamba kwa sasa wanaendesha uchunguzi wao kwa siri ili kuwabaini wahalifu.

 “Unapoweka hadharani kila kitu unaweza kuwafanya wengine wakimbie, kwa hiyo tunafanya hivyo kwanza hadi tutakapowakamata wote,” alieleza Kamanda huyo wa Polisi wa Kusini Unguja.

 Kufuatia tukio hilo Chama cha Wanasheria Wanawake (ZAFELA) pamoja na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake (TAMWA) Zanzibar wanasikitika kupoteza mwanaharakati mkubwa wa masuala ya kijinsia na kulitaka Jeshi la Polisi kufanya kazi kwa ufanisi ili kuhakikisha watuhumiwa wanakamatwa na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.

Mzuri Issa, ambaye ni Mratibu wa TAMWA Zanzibar  alisema kuwa kifo cha  Zaituni ambaye alikuwa Mwenyekiti wa Mtandao wa Kupinga Ukatili wa Kijinsia Mkoa wa Kusini Unguja (MKUKKU), kimekuwa pigo kubwa katika  harakati za kupambana na vitendo hivyo vya ukatili wa kijinsia pamoja na kutafuta usawa wa kijinsia kwa ujumla.

“Hili ni tukio la pili kumtokea Zaituni katika kipindi cha miaka miwili, ambapo tukio la kwanza lilihusisha kuvamiwa nyumbani kwake, kupigwa na kuibiwa fedha mwaka jana,” alieleza Mzuri.

Jamila Mahmoud, Mkurugenzi wa ZAFELA, alisema wahusika wanatakiwa kusakwa  nakuchukuliwa hatua zinazostahili.


No comments:

Post a Comment

Pages