HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

December 28, 2016

WALIOFAULU NI LAZIMA WAENDE SEKONDARI – MAJALIWA

*Asema atafuatilia ajue kwa nini kuna tozo kwenye maghala ya Serikali

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali haitavumilia kuona mamia ya vijana waliofaulu mitihani ya darasa la saba na kuchaguliwa kuingia kidato cha kwanza wanabaki nyumbani eti kwa kuwa hakuna madarasa ya kutosha.

“Serikali haitaridhika kuona vijana waliofaulu vizuri wanashindwa kwenda kidato cha kwanza. Halmashauri zilijua tangu mapema ni wanafunzi wanaenda shule za msingi kwa hiyo inataka kuona wote waliofaulu wanakwenda sekondari kwa asilimia 100,” amesema.

Ametoa kauli hiyo leo mchana wakati akizungumza na viongozi na watendaji wa mkoa wa Lndi mara baada ya kupokea taarifa ya mkoa huo kwenye Ikulu ndogo wilayani Nachingwea. Waziri Mkuu amewasili wilayani Nachingwea akiwa njiani kuelekea Ruangwa kwa mapunziko ya mwisho wa mwaka.

Amesema Serikali ya awamu ya tano imedhamiria kutoa elimu ya bure kwa kila mtoto sasa iweje watoto wengine wanafaulu na wanashindwa kujiunga na elimu ya sekondari. “Tumesema elimu ni bure hakuna sababu ya kufanya wengine wasiende shule wakati azma ya Serikali ni kutoa elimu ya bure. Hakikisheni wote wanaingia katika chaguo la kwanza,” amesema.

Amewataka Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Halmashauri ambazo zimefaulisha wanafunzi lakini hazina madarasa na madawati ya kutosha warudi mezani na kujipanga upya ili kuhakikisha wanafunzi wote waliofaulu wanapangwa na kuanza na wenzao katika chaguo la kwanza kwani wakisubiri chaguo la pili wanakuwa wamechelewa.

“Kama tumepokea vijana wengi kwenye udahili wa kidato cha kwanza, ni dhahiri kuwa ,tutapata Vijana wengi watakaomaliza kidato cha nne. Sote tunajua kuna agizo la kila tarafa kuwa na sekondari moja ya kidato cha tano na sita, nataka utekelezaji wa agizo hili usimamiwe kuanzia sasa.”

“Tafuteni moja kati ya shule kwenye tarafa zenu na ipandishwe hadhi kwa kuwekewa miundombinu inayotakiwa ya bwalo, jiko, mabweni, mifumo ya maji, madarasa na vyoo vya kutosha,” amesema.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema atafuatilia ili abaini ni kwa nini taasisi ya maghala ya Serikali inadai tozo kwa wakulima wanaohifadhi mazao kwenye maghala hayo.

Waziri Mkuu amesema atapitia sheria ya kuanzishwa kwa taasisi hiyo ili kuona kama inaruhusu tozo hizo na kuangalia sheria gani inawaruhusu kutoza kodi. Alihoji inakuwaje taasisi ya Serikali inatoza tozo kwenye maghala ambayo yamejengwa na wananchi.

Akitoa mfano kuhusu ghala la Liwale, Waziri Mkuu amesema: “Kuna viagency vimeanzishwa kazi yao ni kutoza mapato tu. Inakuwaje kunakuwa na taasisi imekaa tu na kuanza kutoza tozo kwa wananchi wanaotumia facility za Serikali. Sheria ya kutoza tozo imetokana na nini na hizo zinakwenda kwa nani, je srikali imeanza kufanya biashara?,” alihoji.

“Nimepata taarifa kuwa walikuja kuzuia mazao yasitoke hadi wao walipwe, hapana huu siyo utaratibu. Ni kwa nini tuwanyang’anye fedha wale waliojenga ghala? Wao walijenga ghala kutokana na ubunifu halafu unasema unawapa sh. 7/- kwa kilo wakati wewe umetoza sh.25/- kwa kilo moja. Hapana hilo halikubaliki,” amesisitiza.

Waziri Mkuu amesema kama Serikali inaruhusu kuwepo kwa tozo hizo kwa jambo ambalo wananchi wamelibuni wenyewe, basi ilipaswa kudai kodi na hiyo kodi ilitakiwa kukusanywa na Mamlaka ya mapato Tanzania (TRA) na siyo vinginevyo.

Waziri Mkuu amesema atafuatilia wakala mbalimbali walioanzishwa kwenye wizara kwani kuna nyingine zinafanya kazi ambazo zilistathili kufanywa na idara kwenye wizara mama.

                            
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMANNE, DESEMBA 27, 2016.

No comments:

Post a Comment

Pages