HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

January 05, 2017

CCM YAZINDUA KAMPENI DIMANI

Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana akimnadi Mgombea wa Ubunge jimbo la Dimani, Juma Ali Juma, katika uzinduzi wa kampeni za Uchaguzi mdogo wa Ubunge katika jimbo hilo, mjini Zanzibar. (Picha na Bashir Nkoromo).

Na Talib Ussi, Zanzibar
PAZIA la Kampeni za uchaguzi limefunguliwa leo kwa Chama cha Mapinduzi (CCM) kuanza kutupia madongo viongozi wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), katika uchaguzi Mdogo wa Jimbo la Dimani Unguja.
Akizungumza katika uwanja wa Kombeni, Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana alieleza kuwa chama chake kitashinda kwa sababu wana tabia ya kubadilisha viongozi kila baada ya miaka 10 wanapoingia kwenye uchaguzi.
“Sasa hawa wapinzani wetu wana mgombea wao mmoja huyo hawabadilishi, hata hao wananchi washamchoka, sasa kwa tabia yao tutawashinda siku zote,” alisema Kinana.
Akimtaja kwa Jina katibu Mkuuwa chama cha wananchi CUF Maalim Seif Sharif Hamad kuwa amekuwa akiwanyima CUF ushindi kwa sababu chaguzi zote anagombea yeye.
Katika kampeni hizo Jina la maalim Seif lilitawala kama vile yeye ndie mgombea wa chama hicho na kutumia nafasi ndogo kumnadi mgombea wa CCM.
Akimnadi mgombea wa CCM, Juma Ali Juma, Kinana alitumia uwanja huo kumuomba Said Salim Bakhresa kuwaajiri vijana wa Dimani katika viwanda vyake kwa sababu Serikali haina uwezo kujenga viwanda.
"Tunamuomba mwekezaji wetu Bakhresa, vijana wetu hawa unawaona hawana ajira, wafanyie mpango na wao wapate nafasi ili waendeshe familia zao," alisema.
Sambamba na hilo Kinana alimtaka Mbunge huyo mtarajiwa akifanikiwa kupata Ubunge, asiwe mwenye kutembelea gari, bali atembee kwa miguuu ili wapiga kura wake wamuone.
“Ukichaguliwa pita katika vijiwe vyote uwasikilize vijana wenzako shida zao na atakaekuomba shilingi elfu 10 usimwambie kuwa huna, mpatie angalau elfu tatu, mwambie kwa kipindi hicho ndio ulizo nazo,” alisema Kinana.
Aidha alimwambia mgombea huyo kuwa asiwe na kutumia lugha ya mchakato wakati anapoelezwa kero za jimbo lake.
“Wanapokuja wapiga kura wako Nyumbani usiwafukuzee, wasikilize na kabla ya kuwasikiliza wapikie chai, halafu uwasikilize kwa umakini."
Awali Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Vuai Ali Vuai, aliwataka wana CCM kufanya kampeni za kistaarabu ili kuweka mustakabali bora wa ushindi wao.
“Sisi ndio tunaotunza amani kwa hiyo tuiswape wapinzani wetu nafasi ya kusema, tufanyeni kampeni za amani” alieleza Vuai.
Kwa Upande wa Katibu wa NEC, Itikadi na Uwenezi Humphrey Polepole aliwataka wana CCM kufuata kasi ya Rais John Magufuli yenye kauli mbiu ya hapa kazi tu ili waweze kushinda tena jimbo hilo.
“Msishuhulishwe na wapinzani hawana muelekeo chama cha mapinduzi ndio imaraa na chenye muelekeo wa maendeleo” alieleza Pole Pole.
Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi aliwataka wanachama hao na wapigakura kwa ujumla kuangalia mfano wa Pemba ambako alisema miaka yote wametawala wapinzani lakini hakuna maendeleo yanayonekana.
Uchaguzi huo mdogo umekuja baada ya aliyekuwa Mbunge wa Jimbo hilo Hafidh Ally Tahir kufariki mwishoni mwa mwezi wa Novemba mwaka jana ambapo vyama 11 vinashiriki.

No comments:

Post a Comment

Pages