HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

March 22, 2017

WAZIRI MKUU AHAMASISHA WAWEKEZAJI KUJA NCHINI

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa ametembelea kiwanda cha kusindika samaki aina ya jodari na kuwakaribisha viongozi wa kiwanda hicho kuja nchini kuangalia maeneo ya uwekezaji wa viwanda vya samaki.

Amesema Serikali imeweka sera nzuri za uwekezaji na pia ina maeneo mengi na mazuri kwa ajili ya uwekezaji wa viwanda vya samaki, ambayo ni bahari, mito na maziwa ambayo aina mbalimbali za samaki.

Waziri Mkuu amesema hayo jana jioni (Jumanne, Machi 21,2017) wakati alipotembelea kiwanda cha samaki cha Mer des Mascareignes kilichoko  jijini Port Louis nchini Mauritius.

“Tanzania kuna fursa nyingi za uwekezaji hasa kutokana na mazingira yake. Mnaweza kuja kuwekeza kwenye viwanda vya usindikaji wa samaki tuna bahari, mito na maziwa yenye samaki wa aina mbalimbali,” alisema.

Waziri Mkuu alisema Serikali imedhamiria kuimarisha uchumi wake kupitia sekta ya viwanda ili kuongeza tija kwa Taifa na kwa wananchi kiujumla hivyo wanahitaji wawekezaji waliotayari kuja kuwekeza nchini.

Kwa upande wake Waziri wa Fedha na Mipango wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Dkt. Khalid Salum Mohammed alisema Tanzania inahitaji wawekezaji watakaowekeza kwenye uvuvi wa kina kirefu na ujenzi wa viwanda vya samaki.

Dkt. Khalid alisema lengo la uwekezaji huo ni kukuza uchumi wa Taifa pamoja kupanua soko la ajira na kuondoa umaskini miongoni mwa wananchi wake.

Naye Meneja Mkuu wa kiwanda hicho, Bw. Patrick Hill alisema wamefurahi na mualiko wa kuja Tanzania kwa ajili ya kuangalia fursa na uwekezaji na kwamba wako tayari kushirikiana na Serikali.

Alisema kampuni yao inajishughulisha na usindikaji wa samaki aina moja tu ya jodari na wananunua kutoka kwa makampuni makubwa ya uvuvi huku wateja wao wakubwa wakiwa ni bara la Ulaya.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu alitembelea kiwanda kingine cha  Chantier Naval Del`Ocean Indien Limited (CNOI) ambacho kinatengeneza na kukarabati meli , boti na pantoni na kujionea uwezo mkubwa walionao, ambapo Watanzania wanaweza kuja kujifunza.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMATANO, MACHI 22, 2017.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, akipata maelezo kutoka kwa Bibi Veroniqu Gorrioch kuhusu utengeneza na ukarabati wa meli, pantoni na boti wakati alipotembelea kiwanda cha kutengeneza na kukarabati meli, pantoni na boti cha Contier Naval Del' Oceaniindien Limited (CNO 1 Company Limited) cha Mauritius Machi 21, 2017. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu). 
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, akipata maelezo kutoka kwa Bibi Veroniqu Gorrioch kuhusu utengeneza na ukarabati wa meli, pantoni na boti wakati alipotembelea kiwanda cha kutengeneza na kukarabati meli, pantoni na boti cha Contier Naval Del' Oceaniindien Limited (CNO 1 Company Limited) cha Mauritius.
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akitembelea kwanda cha kutengeneza na kukarabati meli, boti cha pantoni cha Contier Naval Del' Oceaniindien Limited (CNO 1 Company Limited) cha Mauritius.

No comments:

Post a Comment

Pages