HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

April 12, 2017

RAIS DK. MAGUFULI AWEKA JIWE LA MSINGI UJENZI WA RELI YA KISASA STANDARD GAUGE KUTOKA DAR HADI MOROGORO

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli, leo tarehe 12 Aprili, 2017 ameweka jiwe la msingi la ujenzi wa sehemu ya kwanza ya reli ya kati kwa kiwango cha kisasa (Standard Gauge) itakayoanzia Dar es Salaam hadi Morogoro, yenye urefu wa kilometa 300 zinazojumuisha vituo vya kupishana treni na vituo vya abiria na mizigo.
Sherehe za uwekaji jiwe la msingi zimefanyika Pugu Jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo, Mke wa Rais Mama Janeth Magufuli, Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa Mnyaa, Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Bajeti Mhe. Hawa Ghasia, Mwenyekiti wa Kamati ya kudumu ya Bunge ya Miundombinu Mhe. Prof. Norman Sigalla King, Mabalozi wa nchi mbalimbali, wawakilishi wa taasisi za kimataifa na viongozi wa Mkoa wa Dar es Salaam.
Reli inayojengwa itakuwa na uwezo wa kubeba mizigo yenye uzito wa tani 35 kwa ekseli moja, itasafirisha abiria kwa mwendokasi wa hadi kilometa 160 kwa saa, mizigo kwa mwendokasi wa hadi kilometa 120 kwa saa na itakuwa na uwezo wa kusafirisha jumla ya tani milioni 17 za mizigo kwa mwaka, ikilinganishwa na reli nyembamba iliyopo sasa iliyojengwa mwaka 1912 ambayo inasafirisha abiria kwa mwendokasi wa kilometa chini ya 30 kwa saa, inabeba tani 13 kwa ekseli moja na ina uwezo wa kubeba jumla ya tani milioni 5 tu za mizigo kwa mwaka.
Sehemu ya kwanza ya ujenzi wa reli hiyo inayofanywa na kampuni ya Yapi Merkezi ya Uturuki kwa kushirikiana na Motaengil Africa imepangwa kuchukua muda wa miezi 30 kuanzia sasa kwa gharama ya Shilingi Trilioni 2.7 na itafuatiwa na sehemu nyinyine nne zitakazounganisha reli kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza kwa urefu wa jumla ya kilometa 1,219.
Akitoa taarifa kwa Mhe. Rais, Mtendaji Mkuu wa Kampuni hodhi ya rasilimali za reli nchini (RAHCO) Bw. Masanja Kadogosa amesema reli hiyo itakuwa na uwezo wa kubeba treni inayovuta mabehewa 100 ya mizigo yenye urefu wa kilometa 2 kwa mpigo na kwamba mizigo itakayobebwa na treni moja ni sawa na mizigo ambayo ingebebwa na malori 500.
Ameongeza kuwa kupitia reli hiyo abiria wataweza kusafiri kati ya Dar es Salaam na Morogoro kwa muda wa saa 2 na dakika 50
Mhe. Rais Magufuli amesema Watanzania wana kila sababu ya kujivunia kuanza kwa ujenzi wa reli hiyo kwa kuwa itasaidia kurahisisha usafiri wa abiria na mizigo ndani ya nchi na kwenda nchi jirani za Rwanda, Burundi, Uganda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, itazalisha ajira za moja kwa moja kwa Watanzania 600,000 na itasadia kuimarisha uchumi.
Mhe. Dkt. Magufuli amesema pamoja na kuanza kwa ujenzi wa kilometa 300 za kuanzia Dar es Salaam hadi Morogoro, Serikali imeelekeza jitihada zake kuanza ujenzi wa sehemu ya pili ya kuanzia Morogoro hadi Dodoma yenye urefu wa kilometa 336 na kwamba Serikali ya Uturuki imeonesha nia ya kushirikiana na Tanzania kujenga sehemu hiyo.
Kwa wakazi wa Dar es Salaam, Mhe. Rais Magufuli amesema katika kipindi kifupi Serikali ya Awamu ya Tano imechukua hatua madhubuti za kuboresha Jiji kama alivyoahidi zikiwemo kujenga barabara za juu katika makutano ya barabara maeneo ya TAZARA na Ubungo (Flyover), kujenga daraja la baharini litakalounganisha Agha Ghan na Coco Beach, kujenga barabara za mzunguko (Ring roads) na kununua ndege kwa ajili ya Shirika la Ndege Tanzania (ATCL).
Pamoja na kuwapongeza wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kupitisha bajeti iliyowezesha kuanza kwa ujenzi wa reli ya kati kwa kiwango cha kisasa, Mhe. Rais Magufuli amewaomba Watanzania wote kuendelea kuunga mkono juhudi hizi kubwa na muhimu kwa maendeleo na amewataka kujiepusha na mijadala isiyo na tija katika maendeleo.
 Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es Salaam
12 Aprili, 2017
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa na Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa pamoja na Mkewe Mama Janeth Magufuli akikata utepe kuashiria uzinduzi wa Ujenzi wa Reli ya Kisasa Standard Gauge itakayoanzia jijini Dar es Salaam hadi mkoani Morogoro na baadaye kuendelea hadi mikoa ya Kigoma na Mwanza.
 Picha namba 2. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa na Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mbarawa akiweka jiwe la msingi Ujenzi wa Reli ya Kisasa Standard Gauge itakayoanzia jijini Dar es Salaam hadi mkoani Morogoro na baadaye kuendelea hadi Kigoma na Mwanza.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiangalia majina ya baadhi ya wataalamu mbalimbali waliohusika katika mchakato wa Ujenzi huo wa Reli ya Kisasa Standard Gauge itakayoanzia jijini Dar es Salaam hadi mkoani Morogoro na baadaye kuendelea hadi Kigoma na Mwanza. Wakwanza kulia ni Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hodhi ya Rasilimali za Reli (RAHCO) Masanja Kadogosa akiwa ameshika majina hayo.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiangalia majina ya baadhi ya wataalamu mbalimbali waliohusika katika mchakato wa Ujenzi huo wa Reli ya Kisasa Standard Gauge itakayoanzia jijini Dar es Salaam hadi mkoani Morogoro na baadaye kuendelea hadi Kigoma na Mwanza. Wakwanza kulia ni Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hodhi ya Rasilimali za Reli (RAHCO) Masanja Kadogosa akiwa ameshika majina hayo.
Mke wa Rais Mama Janeth Magufuli akichota mchanga na kuweka kama ishara ya kushiriki katika ujenzi huo wa Reli ya Kisasa Standard Gauge itakayoanzia jijini Dar es Salaam hadi mkoani Morogoro na baadaye kuendelea hadi Kigoma na Mwanza 
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiangalia kibao cha jiwe la msingi cha Ujenzi wa Reli ya Kisasa Standard Gauge itakayoanzia jijini Dar es Salaam hadi mkoani Morogoro na baadaye kuendelea hadi Kigoma na Mwanza
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa na Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mabarawa, Mama Janeth Magufuli wakimsikiliza Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa RAHCO Masanja Kadogosa wakati akielezea kuhusu ujenzi wa Reli ya Kisasa Standard Gauge itakayoanzia jijini Dar es Salaam hadi mkoani Morogoro na baadaye kuendelea hadi Kigoma na Mwanza
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa na Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano Profesa Makame Mabarawa wakati akipita katika katika ya mfano wa Reli hiyo itakayojengwa.  
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwapungia mkono wananchi waliohudhuria sherehe za uwekaji wa jiwe la msingi Ujenzi wa Reli ya Kisasa Standard Gauge itakayoanzia jijini Dar es Salaam hadi mkoani Morogoro na baadaye kuendelea hadi Kigoma na Mwanza
Mfano wa Reli hiyo ya Kisasa ya Standard Gauge SGR itakayojengwa kuanzia Dar es Salaam hadi Morogoro na baadae kuendelea hadi mikoa ya Mwanza na Kigoma. 
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akisalimiana na Kaimu Mtendaji Mkuu wa RAHCO Masanja Kadogosa wakati akielekea kuweka jiwe la Msingi ujenzi wa Reli hiyo ya Kisasa.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akihutubia kabla ya kuweka jiwe la Msingi ujenzi wa Reli hiyo ya Kisasa.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akifurahia jambo na Mufti Mkuu wa Tanzania Shekhe Abubakary Zubeiry mara baada ya kuweka jiwe la Msingi katika eneo la Pugu jijini Dar es Salaam.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akimpongeza msanii Mrisho Mpoto mara baada ya kuweka jiwe la msingi katika ujenzi huo wa Reli ya Kisasa Pugu jijini Dar es Salaam. 
 Mfano wa Reli hiyo ya Kisasa ya Standard Gauge SGR itakayojengwa kuanzia Dar es Salaam hadi Morogoro na baadae kuendelea hadi mikoa ya Mwanza na Kigoma. PICHA NA IKULU

No comments:

Post a Comment

Pages