HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

April 21, 2017

TAASISI YA VICTORIA YAZINDULIWA NA KUTOA MAFUNZO KWA WAJANE

Picha mbalimbali zikionesha matukio wakati wa uzinduzi wa Taasisi ya Victoria Foundation uliofanyika hivi karibuni katika mji wa Geita ulioenda sabambamba na utoaji vyeti kwa washiriki wa mafunzo ya ujasiriamali.

Mwandishi Wetu

MAFUNZO ya ujasiriamali yametolewa kwa wanawake wajane na wasiojiweza wa mkoa wa Geita kupitia mfuko wa Victoria Foundation unaomilikiwa na mbunge wa viti maalum CCM, Vicky Kamata.

Mafunzo hayo yalitolewa kwa lengo la kupunguza pengo la elimu ya masuala ya fedha kwa wanawake hao kwa kuwafundisha mbinu mbali mbali za biashara, namna ya kuweka akiba na kulipa mikipo.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mafunzo hayo, Mkuu wa mkoa wa Geita, Meja Jenerali Mstaafu Ezekiel Kyunga alimpongeza Kamata kwa jitihada zake kwa kuinua wanawake hususani wajane na wasiojiweza kiuchumi na kuwataka wanawake kujenga utamaduni wa kufuatilia taarifa mbali mbali kuhusiana na masuala ya fursa za kibiashara ili kuzitumia katika kupanua wigo wa shughuli zao.

Alisema wanawake wengi nchini wanashindwa kusonga mbele kibiashara kwa kuwa wanakosa taarifa ambazo zingetumiwa kuwawezesha kusonga mbele na kujikwamua kiuchumi.

"Ni wakati sasa kwa wanawake nchini kutafuta taarifa zitakazoinua biashara, mafunzo kama haya mmeyapata bure myatumie vema kuhakikisha mnatimiza malengo yenu.”alisema.

Kwa upande wa muandaaji wa mafunzo hayo, Vicky Kamata alisema mfuko wake mbali na kutoa misaada mbali mbali kwa walemavu, ni wakati sasa wa kusaidia elimu kwa wanawake na kuwawezesha mitaji ili waweze kufikia lengo.

“Naamini mwanamke ni jeshi kubwa, ukimuwezesha mwanamke mmoja umewezesha jeshi kubwa lililopo nyuma yake hata watoto watasoma vizuri.”alisema Kamata

Awali  kupitia mfuko huo wa Victoria Foundation, awamu wa kwanza ya utekelezaji wa ahadi zake kwa wakazi wa Geita waliomsaidia kuchaguliwa kwake kuwa mbunge kupitia CCM , Kamata alitoa misaada ya  vyakula, mavazi, magodoro na viti vya walemavu (Wheel Chair) 30 kwa wakazi wa tarafa ya Bugando.

Alisema kupitia mfuko wa Victoria Foundation  wakazi wa Geita watanufaika kwa misaada mbali mbali itakayowawezesha watu hususani wanawake wajane na yatima na wale wasiojiweza kuondokana na adha walizonazo na kufurahia maisha kama watu wengine.
Source:DailyNews-Habarileo Blog

No comments:

Post a Comment

Pages