HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

May 12, 2017

Amua mumewe kwa wivu

Na Tallibu Ussi

MTU mmoja anaejulikana kwa jina la Tani Ali Tani (41) mkaazi wa Kizimbani Wete amefariki dunia baada ya kuchomwa kisu na mkewe Khadija Mbarouk (44), huko katika shehia ya Kizimbani Wilaya ya Wete Mkoa wa Kaskazini Pemba.


Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kaskazini Pemba Haji Khamis Haji amesema tukio hilo limetokea jana (juzi) majira ya 2:30 usiku katika eneo la Kizimbani.


Kamanda Haji alitaja chanzo cha tukio hilo kuwa ni wivu wa mapenzi.


Alisema kuwa, marehemu alijeruhiwa baada ya kuchomwa kisu na mkewe katika mguu wake wa kushoto na kutokwa na damu nyingi ambayo ndio iliyosababisha kifo chake.


"Khadija alikwenda nyumbani kwa mke mwenziwe alipokuweko mumewe (marehemu) na kutaka kuzungumza nae, ambapo hapo waligombana na ndipo mwanamke huyo alipochukua hatua ya kunchoma kisu mumewe", alisema Kamanda Haji.


Alisema kuwa, mara baada ya kujeruhiwa alikimbizwa katika hospitali ya Wete kwa ajili ya matibabu, ambapo ilipofika saa 9:00 usiku alifariki.


Kamanda huyo alisema kuwa kwa sasa ntuhumiwa yuko chini ya ulinzi na upelelezi utakapokamilika atafikishwa mahakamani kujibu shitaka linalomkabili.


Hivyo aliwataka wananchi kuacha kujichukulia sheria mikononi mwao na badala yake wafike katika vyombo husika kuripoti, iwapo kuna kosa la jinai liweze kuchukuliwa hatua za kisheria.


Kwa upande wao wananchi wa eneo hilo, walidai kuwa Khadija alitoka kwake na watoto wake huku akiwa na kisu kwenda kumwita mumewe, ambapo walianza kugombana nje ya nyumba ya mke mwenzake na ndipo alipopandwa na hasira na kumchoma kisu cha mguu mumewe.

No comments:

Post a Comment

Pages