HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

May 06, 2017

SAFARI ZA ATCL MKOANI TABORA ZAZINDULIWA RASMI

 Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Sekta ya Uchukuzi, Dkt. Leonard Chamuriho, wakiwa ndani ya ndege kuelekea katika uzinduzi wa safari za ndege za Kampuni ya Ndege ya Tanzania (ATCL), mkoani Tabora.
 Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani, akihutubia wananchi wa Tabora (hawapo pichani), waliohudhuria uzinduzi wa safari za ndege za Kampuni ya Ndege ya Tanzania (ATCL), mkoani humo.
 Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Sekta ya Uchukuzi, Dkt. Leonard Chamuriho, akizungumza wakati wa uzinduzi wa safari za ndege za Kampuni ya Ndege ya Tanzania (ATCL), mkoani Tabora.
 Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani, akizungumza jambo na Mkuu wa Mkoa wa Tabora Bw. Aggrey Mwanri, wakati wa uzinduzi wa safari za Ndege za Kampuni ya Ndege ya Tanzania (ATCL), mkoani humo.
 Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani, na Mkuu wa Mkoa wa Tabora Bw. Aggrey Mwanri, wakikata keki kama ishara ya kuzindua rasmi safari za Ndege za Kampuni ya Ndege ya Tanzania (ATCL), mkoani humo.
 Baadhi ya viongozi na wabunge wakiingia kwenye ndege aina ya Bombardier Dash 8 Q400 ya Kampuni ya Ndege ya Tanzania (ATCL), iliyotua kwa mara ya kwanza mkoani Tabora katika uzinduzi wa safari za ndege mkoani humo.
Baadhi ya wabunge wakirejea mkoani Dodoma mara baada ya uzinduzi wa safari za ndege za Kampuni ya Ndege ya Tanzania (ATCL), mkoani Tabora. Uzinduzi huo ulifanywa na Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani.

Kampuni ya Ndege ya Tanzania (ATCL), imeanzisha safari zake kutoka Tabora kwenda mikoa ya Dodoma na Dar es Salaam kwa lengo la kurahisisha huduma za usafirishaji wa abiria na mizigo katika mikoa hiyo na mikoa jirani.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa safari za ndege za kampuni hiyo mkoani Tabora, Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani, amesema kuwa  kuanzishwa kwa safari hizo katika mikoa hiyo kutatanua wigo wa kibiashara na kukuza uchumi kupitia sekta  mbalimbali ikiwemo za utalii na kilimo.
“Naamini wananchi wa mkoa wa Tabora na mikoa ya jirani, sasa mtanufaika kwa ujio wa ndege hii, matumaini yangu kwamba mtatumia usafiri huu ambao hautumii muda mrefu katika kurahisisha shughuli zenu za kibiashara na kijamii”, amesema Eng. Ngonyani.
Aidha, Naibu Waziri Ngonyani amewataka wananchi wa mkoa wa Tabora kutumia fursa ya ujio wa ndege hiyo kama chachu ya kuleta maendeleo katika mkoa huo.
Sambamba na hilo Eng. Ngonyani, amesema kuwa katika kuhakikisha usafiri wa anga unaimarika nchini Serikali itaongeza ndege nyingine tatu katika mwaka wa fedha 2017/18 ambapo hadi kufikia mwezi Julai mwakani ndege hizo zitakuwa zimewasili.
Naibu Waziri Ngonyani amefafanua kuwa ndege mbili kati ya hizo zitakuwa za masafa ya kati aina ya CS 300 ambazo zina uwezo wa kubeba abiria 132 kila moja na ndege moja ya masafa marefu aina ya Boeing 787 Dreamliner yenye uwezo wa kubeba abiria 262.
Katika hatua nyingine, Eng. Ngonyani amewaagiza wafanyakazi wa ATCL kufanya kazi kwa juhudi, uadilifu na weledi kwa lengo la kuijengea sifa kampuni hiyo na kuvutia wateja ili kujiimarisha katika soko la ushindani.
Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Sekta ya Uchukuzi, Dkt. Leonard Chamuriho, amewataka wananchi wa mkoa huo kutumia fursa ya kupata usafiri wenye gharama nafuu na wa muda mfupi.
Naye, Mkuu wa Mkoa huo Bw. Aggrey Mwanri, amewataka wananchi wa mkoa huo na mikoa ya jirani kujitokeza kwa wingi kupata huduma ya usafiri huo ambao walikuwa wakiusubiri muda mrefu.
Uzinduzi wa safari za ndege mkoani humo ni moja ya hatua za kuboresha usafiri wa anga nchini ambapo Serikali kupitia ATCL ina mpango wa kuanzisha safari katika mikoa mingine na nchi jirani ili kurahisisha huduma za kijamii na kibiashara. 
Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.

No comments:

Post a Comment

Pages