HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

May 10, 2017

WAKUU WA WILAYA, WAKURUGENZI ZINGATIENI MIPAKA YA MADARAKA YENU-MAJALIWA

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Halmashauri nchini kuzingatia mipaka ya madaraka yao na kuhakikisha hatua wanazochukua katika utendaji wao zinafuata  Sheria ,Kanuni na Taratibu katika Utumishi wa Umma.

Ametoa kauli hiyo leo (Jumanne, Mei 9, 2017) wakati akifungua mafunzo kwa Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Halmashauri za Wilaya katika  ukumbi wa Hazina mjini Dodoma.

Amesema viongozi hao wanatakiwa kusimamia kikamilifu nidhamu katika Utumishi wa Umma kwa sababu wenyewe ni kioo katika kuishi kwa kuzingatia miiko ya Utumishi wa Umma.

Aidha,Mh. Waziri Mkuu amesema mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo na kuendelea kuwaimarisha zaidi katika kusimamia shughuli za Serikali na maendeleo kwenye maeneo yao.

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amewataka viongozi hao kutoa kipaumbelea katika kufuatilia na kusimamia kwa makini sekta za afya, kilimo, elimu na maji kwa kuwa ndizo zinazogusa zaidi maisha ya wananchi .

Pia amewaelekeza wasimamie na kuziba mianya yote ya upotevu wa dawa katika vituo vya kutolea huduma za afya na kudhibiti migogoro ya wakulima na wafugaji pamoja na kusimamia usafi na utunzaji wa mazingira katika maeneo yao.

Kwa upande wake Naibu Waziri Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa-TAMISEMI, Mheshimiwa Suleiman Jafo amesema lengo la mafunzo hayo ni kuhakikisha viongozi hao wanapata mafanikio makubwa katika utendaji wao wa kazi ili Serikali iweze kupata tija.

Awali Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi, Profesa Joseph Semboja alisema wametoa mafunzo kwa viongozi hao ili kuwajengea uwezo wa kuongoza kwa kuwa mazingira ya kufanyia kazi na mbinu za kungoza zinabadilika.

Alisema mafunzo hayo yatatolewa kwa awamu nne kupitia kanda nne tofauti ambapo awamu ya kwanza imeanza na kanda ya kati na imehusisha mikoa sita ya Dodoma, Kigoma, Katavi, Tabora, Morogoro na Singida na awamu nyingine zitakamilika mwishoni mwa mwezi Agosti mwaka huu.

 IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
S. L. P. 980,
DODOMA.
JUMANNE, MEI 9, 2017.

No comments:

Post a Comment

Pages