HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

June 03, 2017

KANDA YA ZIWA YAFANYA VIZURI UHAKIKI WA MIZANI YA PAMBA

  3,070 Iliyo Hakikiwa yakutwa Salama.
Na Atley Kuni - Mwanza.
Jumla ya mizani 3,070 Iliyo Hakikiwa katika mikoa ya kanda ya ziwa kwa ajili ya matayarisho ya ununuzi wa pamba kwa msimu wa 2017/2018 imekutwa salama mara baada ya kuhakikiwa na wakala wa Vipimo nchini.
Akizungumza nami Jijini Mwanza, kaimu Meneja Sehemu ya Elimu, Habari na Mawasiliano Bi. Irene John, amesema, Wakala wa vipimo Tanzania ( WMA) chini ya usimamizi wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji imeendelea kutoa elimu  kwa wakulima  pamoja na kuhakiki mizani itakayotumika kununulia zao la Pamba ikiwa ni maandalizi ya msimu wa ununuzi wa Pamba kwa mwaka huu.
Bi. Irene amesema,  Dhumuni kuu  la utoaji elimu  kwa wakulima wa zao la Pamba  Kanda  ya Ziwa  ni kuwawezesha  wakulima  kutambua mizani iliyosahihi                          (inayoruhusiwa kwa biashara)  na ile iliyochezewa (isiyoruhusiwa kwa biashara)  ili waweze kujilinda wenyewe pindi maafisa vipimo wanapokuwa hawapo katika vituo vya kuuzia Pamba yao, lakini pia ni kuwawezesha wakulima kupata  faida ya thamani kamili ya jasho lao.
 Ameongeza kuwa, katika maandalizi ya msimu mpya wa ununuzi wa Pamba zaidi ya mizani  1,402 imekaguliwa  katika mkoa wa Shinyanga,  mkoa wa Simiyu  wamekagua zaidi ya mizani 302,  mkoa wa Geita jumla ya mizani 40 tayari imekaguliwa,  ilihali katika mkoa wa Mwanza  wamekagua mizani 448, mkoa wa Mara  mizani 690,  mkoa wa Tabora wamekagua mizani 164    pamoja na mkoa wa Kagera   wamekagua jumla ya mizani 24 ikiwa ni maandalizi ya ununuzi wa zao la Pamba.
Katika hatua nyingine Irene amesema,  sheria ya Vipimo Sura 340 inawataka Wakala wa Vipimo  kuhakiki na kupiga chapa vipimo vyote vinavyotumika katika biashara ikiwa ni pamoja na  kuweka   sticker kwa kipimo kitakachokuwa tayari kimehakikiwa na kukutwa kikiwa sahihi  ili iwe rahisi kwa wakulima kuona na kutambua mizani iliyokaguliwa na kuruhusiwa kwa biashara kwa mwaka husika.
 “Wakala wa Vipimo nchini itaendelea kufanya ukaguzi wa kushtukiza wakati wowote  baada ya msimu wa ununuzi wa Pamba kuanza ili panapokuwa na malalamiko kutoka kwa wananchi kuhusu uonevu katika mizani yaweze kutatuliwa wa haraka” amesema Irene
Aidha amewataka wakulima wanaolalamikiwa kuweka maji, kokoto pamoja na mchanga kwenye Pamba kwa ajili ya kuongeza uzito waache tabia hiyo mara moja  sababu Sheria ya vipimo ipo na inafanyakazi kwa pande zote mbili muuzaji na mnunuzi wote kwa pamoja hawatakiwi kufanya udanganyifu wowote katika biashara.
Bi Irene hakusita kutaja  faini  itakayotozwa kwa wote watakao banika kufanya udanganyifu “faini itaanzia  laki moja  badala ya elfu kumi kama ilivyo zoeleka hadi milioni ishirini endapo mkosaji atakubali kosa, endapo kesi itafikishwa mahakamani na mlalamikiwa akakutwa kweli alikosa kulingana na ushahidi utakaokuwa umetolewa “ na kusema “mshitakiwa atatozwa faini kuanzia laki tatu hadi milioni hamsini au kifungo cha miaka mitatu au vyote kwa pamoja”.
Irene alisema Tanzania ya viwanda itafanikiwa  endapo Mkulima, Mfanyabiashara watazingatia matumizi ya vipimo sahihi kuanzia maandalizi ya shamba, upandaji wa mazao, utumiaji wa pembejeo, uuzaji, usafarishaji, upokeaji wa mazao, ufungashaji hadi utumiaji wa mazao yenyewe.
 Wakala wa Vipimo itaendelea kutoa elimu kwa  wakulima na wafanyabiashara ili wajue thamani ya kuuza kwa kutumia mizani iliyohakikiwa na Wakala wa Vipimo ikiwa ni pamoja na kumsaidia mkulima kupata fedha kulingana na thamani ya mazao yake, kufanya biashara ya haki na kuepusha migogoro/migongano, kukuza uchumi wa mkulima  mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla
Bi. Irene  alisema "elimu kwa pande zote mbili (Mkulima na Mfanyabiashara)  ni muhimu lakini zaidi kwa mkulima kwani,  mbali ya kutumia muda wake mwingi katika kuandaa shamba, kulima, kupalilia na hata kuvuna bado ameoneka kuwa mnyonge kwenye mazao yake ndiyo maana  kwa sasa tunazunguka Kanda ya Ziwa mikoa inayolima Pamba   kwa wanunuzi na  wakulima kwa ajili ya kutoa elimu  ya matumizi sahihi ya mizani kabla ya uuzaji wa zao la Pamba kuanza.
Afisa huyo amesema kuanzia hatua ya awali ya kuandaa shamba hadi kuvuna mkulima anahitaji matumizi sahihi ya vipimo   lakini wakati wa kuuza mazao, umakini wa  matumizi sahihi ya vipimo unahitajika sana, ambapo kipimo kikiwa sahihi na kikatumiwa kwa usahihi, kitatoa matokeo sahihi kumwezesha muuzaji (mkulima) kupata fedha sawa na thamani ya bidhaa aliyouza.

 Hivyo, nia na lengo la utoaji wa elimu pamoja na  uhakiki mizani  ni kuwasaidia wakulima  kabla ya  msimu wa Pamba  kuanza  wapate elimu ya kutosha hatimaye  mkulima aweze kupata fedha kulingana na thamani ya bidhaa atakayoizalisha na kuwasilisha sokoni. “Mwaka huu tutajitahidi kuongeza elimu zaidi kwa wakulima ikiwa ni pamoja na kuongeza kaguzi za kushutukiza  ili kuwadhibiti baadhi ya wafanyabiashara wasio waaminifu kuchezea mizani kwa lengo la kuwaibia wakulima” alisema  Kaimu Meneja Bi Irene.

No comments:

Post a Comment

Pages