HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

June 08, 2017

WADAU WAKUTANA KUJADILI MFUKO WA KUENDELEZA UBUNIFU VIJIJINI

 Mratibu wa Uanzishwaji wa Mfuko wa Ubunifu Vijijini, Bw. Albert Ngusaru akizungumza kabla ya ufunguzi wa mkutano wa siku moja wa kujadili namna bora ya kuendeleza Mfuko huo.
 Mwezeshaji wa Majadiliano ya Uanzishwaji wa Mfuko wa Ubunifu Vijijini, Bw. Severin Ndaskoi (kushoto) akihimiza jambo wakati wa majadiliano hayo. Kulia ni Meneja wa Hazina na Ukwasi wa TADB, Bibi Beatrice Mrema.
Washiriki wa Mkutano wa Majadiliano ya Uanzishwaji wa Mfuko wa Ubunifu Vijijini wakifuatilia kwa umakini mkutano huo.

Na Mwandishi Wetu,

Wadau kutoka sekta za kilimo na uchumi wamekutana kujadiliana namna bora ya uanzishwaji wa Mfuko wa Ubunifu Vijijini (rural innovation fund) wenye lengo la kuchochea, kuhamasisha na kusaidia uvumbuvi katika maeneo ya maendeleo vijijini, ukopeshaji wa shughuli za kilimo na huduma za taasisi ndogo za kifedha.

Mkutano huo wa siku moja umeandaliwa kwa ushirikiano wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) na Programu ya Miundombinu ya Masoko, Uongezaji Thamani Mazao na Huduma za Kifedha Vijijini (MIVARF).

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mkutano huo, Mwakilishi wa Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa TADB, Bw. Adam Kamanda amesema wadau wana mchango mkubwa wa kutoa maoni yatakayosaidia kuboresha usimamizi wa Mfuko huo ambao utakuwa chini ya TADB.

“Nawaomba tujadili namna bora itakayosaidia ndoto ya Serikali ya kuchagiza upatikanaji wa fedha za gharama nafuu kwa ajili ya kuwasaidia wakulima hasa katika maeneo ya maendeleo vijijini, ukopeshaji wa shughuli za kilimo na huduma za taasisi ndogo za kifedha,” alisema.

Bw. Kamanda ameongeza kuwa uanzishwaji wa mfuko huu unalenga kutekeleza kwa vitendo dhamira ya Serikali ya kutatua changamoto zinazoikabili sekta ya kilimo ambayo ni shughuli kuu kwa Watanzania wengi wanaoishi maeneo ya vijijini.

“Uanzishwaji wa Mfuko huu utasaidia bado ukuaji wa sekta ya maendeleo vijijini ambayo imekuwa ukikabiliwa na changamoto mbali mbali kama vile kiwango kidogo cha uzalishaji; ukosefu wa mbinu na teknolojia za kisasa; matumizi madogo ya umwagiliaji; ukosefu wa mtaji na upatikanaji wa mikopo kwa wakulima,” aliongeza.

Kwa upande wake Mshauri wa Kiufundi wa MIVARF, Bw. Ravi Malik alisema kuanza kazi kwa Mfuko huu kutasaidia changamoto za ukosefu wa masoko ya mazao, miundo mbinu mibovu ya usafirishaji, nishati ya umeme na miundombinu hafifu vijijini hali itakayochochea ongezeko la thamani kwa mazao ya kilimo maeneo ya vijijini.

Bw. Malik aliongeza kuwa Mfuko huo utawezeshwa kwa kupatiwa mtaji wa Fedha za Kimarekani (USD) zipatazo Milioni 5 ambazo zitatolewa kwa ushirikiano wa Serikali ya Tanzania kwa ushirikiano na Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD).

“Fedha hizi zimelenga kukuza ongezeko la upatikanaji wa huduma za kifedha kwa wananchi waishio vijijini kupitia njia mbalimbali za utoaji wa fedha ikiwa ni pamoja na huduma za mitandao ya simu ambazo zimekuwa kiungo muhimu katika kuongeza ushirikishwaji wa kifedha kwa watu wasiotumia huduma za kibenki,” aliongeza.

No comments:

Post a Comment

Pages