HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

June 19, 2017

WAZIRI MWAKYEMBE AWAOMBA WADAU WA MCHEZO WA YOGA KUTOA ELIMU KWA WANANCHI KUHUSU MCHEZO HUO

Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe (katikati waliokaa) akishiriki mazoezi ya Yoga katika maadhimisho ya Mchezo huo hapa nchini yaliyofanyika jijini Dar es Salaam.

Na Shamimu Nyaki–WHUSM

Wadau wa mchezo wa Yoga nchini wametakiwa kutoa elimu ya kutosha kwa wananchi ili wapate kuufahamu na kushiriki kwa ajili ya kuimarisha afya zao na kuongeza ufanisi katika kazi zao za kila siku . 

Hayo yamesemwa na Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Mhe. Dk. Harisson Mwakyembe wakati wa maadhimisho ya siku ya Yoga jana Jijini Dar es Salaam katika uwanja wa uhuru.

“Nimefarijika kuwa sehemu ya maadhimisho haya kwani nilikuwa nafikiri Yoga ni mchezo wa misuli tu lakini leo nimejionea mwenyewe uhalisia wake na jinsi unavyounganisha akili na mwili kwa pamoja, nawaomba muelimishe wananchi mchezo huu ili nao waweze kushiriki.” Alisema Mhe. Mwakyembe.

Aidha Mhe. Mwakyembe amewashauri waandaaji wa mchezo huo kuupeleka Mkoani Dodoma ambapo ndipo makao makuu ya nchi ili kuwapa fursa viongozi wa Serikali na Wabunge kushiriki kwa manufaa ya afya na kuongeza utendaji kazi.

Kwa upande wake Balozi wa India hapa nchini Mhe. Sandeep Arya amesema kuwa Serikali yake itatekeleza ombi la Mhe. Waziri Mwakyembe la kutoa elimu kwa wananchi kuhusu mchezo huo ili kuendeleza ushirikiano baina ya nchi hizo.

Mchezo wa Yoga ni mchezo wa kuchezesha viungo vya mwili lengo lake likiwa ni kuimarisha afya ana akili na huadhimishwa Juni 18 kila mwaka.

No comments:

Post a Comment

Pages