HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

July 28, 2017

RC Rukwa ashirikisha wapinzani katika harambee ya ujenzi wa kituo cha afya

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Zelote Stephen (katikati), akionyeshwa kitanda cha kujifungulia na Mganga Mkuu wa Mkoa, Dk. Boniface Kasululu muda mfupi kabla ya kuvikabidhi kwa Wakuu wa Wilaya. Kutoka kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Kalambo, Julieth Binyura akifuatiwa na Katibu tawala wa Mkoa Bernard Makali. (Picha na Ofisi ya Mkoa).
 
 Na Mwandishi Wetu, Rukwa

Katika kuendeleza dhana ya maendeleo hayana chama Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Kamishna Mstaafu Zelote Stephen amewashirikisha madiwani wa chama cha CHADEMA katika harambee ya ghafla iliyolenga kumalizia ujenzi wa jengo la huduma za afya ya uzazi na mtoto katika kituo cha afya Mazwi, Manispaa ya Sumbawanga.

Harambee hiyo ilifanyika muda mfupi kabla ya Mh. Zelote Kukabidhi jumla ya vitanda vya kujifungulia 16, vitanda vya wagonjwa 80, magodoro 80 pamoja na mashuka 200 kwa wakuu wa wilaya ikiwa ni sehemu ya mgawo wa vifaa hivyo uliofanyika nchi nzima kupitia juhudi za Rais Dk. John Pombe Magufuli katika kuimarisha huduma za uzazi nchini.

Akiongea mbele ya wananchi waliohudhuria katika tukio hilo Mh. Zelote alisema kuwa serikali ya awamu ya tano sio ya maongezi bali vitendo hivyo kuwataka waheshimiwa madiwani sita wakiwemo watatu wa CHADEMA wakiongozwa na Meya wa Manispaa ya Sumbawanga kuchangia ujenzi wa jengo hilo jipya ili kuboresha huduma kwa wananchi waliowachagua.

“Ili Manispaa iwe jiji tunahitaji huduma bora katika kituo hiki hivyo basi, Mimi Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Zelote Stephen nachangia tani tano za “cement” ambayo ni mifuko 100,” alitangulia kusema.

Harambee hiyo ilikusanya ahadi ya vifaa vyenye thamani ya shilingi milioni 5.5 huku jengo hilo likiwa limegharimu Shilingi Milioni 16 hadi kusimama.

Awali akisomewa taarifa kabla ya kuzindua huduma ya kujifungua iliyoanza tarehe 1/7/2017 katika kituo hicho afisa muuguzi Mariam Kidya alieleza kuwa jengo lililopo la huduma ya afya ya uzazi na mtoto lina uwezo wa kuhudumia kina mama 2,327 lakini kwa mwaka 2016/2017 limeweza kuhudumia kina mama 31,257 jambo lililopelekea kuanzisha ujenzi wa jengo jipya ili kuimarisha utoaji wa huduma kwa akina mama.

Aidha Mh. Zelote aliwasisitiza wananchi kuendelea kulipa kodi ili kuendelea kuboresha huduma na kuleta maendeleo katika sekta mbalimbali nchini na kuonya kuwa wale watakaolipishwa ili kupata huduma ya afya ya uzazi na mtoto basi wafike ofisini kwake ili achukue hatua.

“Ndio maana Mheshimiwa Rais amesisitiza sana watu tulipe kodi wote ili kutatua kero mbalimbali za wananchi hususan watu wa hali ya chini.  Nataka nisisitize ulipaji wa kodi ili kazi kama hii na zingine zifanyike.

Kwa upande wake mganga mkuu wa mkoa Dk. Boniface kasululu alipokuwa akisoma taarifa ya huduma ya afya na uzazi ya mkoa, alisifu uamuzi wa Rais Dk. John Pombe Magufuli wa kununua vifaa hivyo kupitia bohari kuu ya dawa (MSD) kwani changamoto hizo zimekuwa zikiwasumbua kwa muda mrefu kuanzia ngazi ya mkoa hadi katika halmashauri.

“Sekta ya afya kukabiliwa na changamoto kadhaa kubwa ikiwa ni upungufu wa vifaa na vifaa tiba muhimu na ufinyu wa miundombinu ya kutolea huduma kwa maana ya majengo, hivyo tunapongeza juhudi za rais wetu mpendwa kutupatia vifaa hivi na tunaahidi kuvitunza ili viweze kuwasaidia kina mama wa mkoa wetu,” Alisema. 

No comments:

Post a Comment

Pages