HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

August 04, 2017

RC Rukwa ashauri Nanenane nyanda za juu kusini kushirikisha nchi za SADC

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa KamishnMstaafu Zelote Stephen ameishauri kamati ya maandalizi ya nanenane nyanda za juu kusini kufikiria kushirikisha nchi za SADC ili kuongeza hamasa na kuleta ushindani kwa watanzania wafahamu yanayofanyika katika nchi za jirani.

Ametoa ushauri alipokuwa akifanya majumuisho baada ya kutembelea mabanda 16 ya bidhaa mbalimbali za kilimo katika maonesho ya nane nane kwa kanda ya nyanda za juu kusini yanayofanyika katika viwanja vya John Mwakangale jijini Mbeya ambapo Mh. Zelote Stephen alikuwa mgeni rasmi wa siku ya tatu tangu ufunguzi wa maonesho hayo.

“Tuachane na mazoea, maonyesho haya yana miaka 25 sasa tuyaboreshe zaidi, isiswe ni mikoa hii tu saba, tupanue wigo, kwakiwa huku ni nyanda za juu kusini basi tufikirie kuzishirikisha nchi za SADC ambazo zitasaidia kubadilishana biashara na teknolojia pamoja na kutafuta masoko,” Alifafanua.

Akisisitiza suala hilo Mh. Zelote alibainisha kuwa nchi ya Tanzania inafikika kwa njia zote, ardhini, majini na angani huku akitaja meli mbili zilizozinduliwa Mkoani Mbeya na Waziri Mkuu Mh. Kasim Majaliwa, treni ya TAZARA pamoja na ndege zinazomilikiwa na nchi yetu. 
  
Aidha amezishauri halmashauri kuanza maandalizi kwa kuwa na siku maalum kwaajili ya maadhimisho hayo kihalmashauri ili kuwapa ujuzi na kujua ubora wa vitu ambavyo vinaweza kupelekwa kwenye maadhimisho ya nanenane kikanda ili kuimarisha ushindani na kumpa kila mwananchi nafasi ya kuelimika ili kuwa na kilimo chenye tija.

Akiunga Mkono Kauli ya Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga Mh. Kilolo Ntila alityekuwemo katika msafara huo alisisitiza kuwa maonesho ya nanenane yanayofanyika kikanda yanalenga watu wenye kipato cha kutoka katika halmashauri zao na kukusanyika jijini Mbeya huku wakulima wasio na uwezo wakikosa elimu inayopatikana kutokana na maonyesho hayo.

“Nikiongezea aliyoyasema Mheshimiwa Mkuu wangu wa Mkoa, kwa nafasi yake namuomba aweze kushawishi haya makampuni makubwa kuweza kusambaza wataalamu wao katika Halmashauri zetu ambapo kuna uhitaji mkubwa wa elimu hii inayotolewa hapa katika viwanja hivi vya nanenane na wao ndio walengwa wakubwa wa shughuli hii,” alisema.

Pamoja na hayo Mh. Zelote alitoa wito kwa wananchi wote wenye nafasi wajitokeze kwa wingi kwenye maonyesho hayo ili waweze kuelimika kutokana na mafunzo mbalimbali yanayotolewa viwanja hivyo vya nanenane na kusifu maandalizi ya sherehe hizo.

No comments:

Post a Comment

Pages