HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

August 18, 2017

TUTAENDELEZA MAHUSIANO YA KIDIPLOMASIA YALIYOJENGWA NA AWAMU ZILIZOTANGULIA-MAJALIWA

 WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Dkt. John Magufuli inayatambua na kuyathamini mahusiano mazuri ya kidiplomasia yaliyojengwa na awamu zilizotangulia baina ya Tanzania na mataifa mbalimbali ikiwemo Jamuhuri ya Cuba na kwamba itayaendelea.

Ametoa kauli hiyo jana jioni (Alhamisi, Agosti 17, 2017), alipozungumza na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Cuba, Bi Anna Teressa mara baada ya kuwasili nchini Cuba kwa ajili ya ziara ya kikazi yenye lengo la kudumisha ushirikiano kati ya nchi hizo mbili.

“Tanzania na Cuba zina historia ya kutosha. Tunatambua mahusiano mazuri yaliyopo kati nchi zote mbili, ambayo yalikuwepo kuanzia Serikali ya Awamu ya kwanza chini ya uongozi wa Baba wa Taifa Hayati Mwl. Julius Nyerere.”

Amesema katika ziara yake hiyo anatarajia kufanya mazungumzo na viongozi mbalimbali waandamizi wa Serikali ya Cuba kwa lengo la kukuza ushirikiano katika sekta za Afya, Elimu, Utalii na Kilimo.

Waziri Mkuu amesema Cuba ni mojawapo kati ya nchi zenye ushirikano wa muda mrefu na Tanzania kisiasa, kijamii, kiafya na kiuchumi.”Mfano katika Sekta ya Afya, madaktari wengi kutoka Cuba walikuwa wanakuja Tanzania kutibu wagonja waliokuwa na maradhi makubwa.”

Pia Waziri Mkuu amesema katika ziara hiyo anatarajia kukutana na Jumuya ya Wafanyabiashara wa Cuba ili kuwaelezea fursa za uwekezaji zilizopo nchini Tanzania hususan  katika Sekta ya Viwanda pamoja na kutangaza vivutio vya utalii vilivyopo nchini.

Kwa upande wake Bi. Anna ambaye alimpokea Waziri Mkuu kwa niaba ya Serikali ya Cuba alitumia fursa hiyo kuishukuru Serikali ya Tanzania kwa kuendelea ushirikiano mzuri baina ya nchi hizo mbili, hivyo alimuhakikishia kwamba wataendelea kuudumisha.

Pia Bi. Anna ametumia fursa hiyo kuupongeza uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Dkt. John Magufuli kwa namna inavyopambana na rushwa, ufisadi, kuhimiza uwajibikaji pamoja na kutetea wanyonge.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU, 
IJUMAA, AGOSTI 18, 2017.

No comments:

Post a Comment

Pages