HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

September 15, 2017

WAZIRI MKUU AWAASA WATENDAJI WA TAASISI ZINAZOSIMAMIA MAZAO YA BIASHARA

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka viongozi wa taasisi zilizopewa dhamana ya kusimamia mazao makuu matano ya biashara ambayo ni ya pamba, tumbaku, korosho, chai na kahawa kutekeleza majukumu yao ipasavyo.

Amesema mazao hayo ni muhimu sana katika kuwezesha mkakati wa Serikali ya Awamu ya Tano wa kufikia uchumi wa viwanda kwani ndiyo mhimili wa kutoa malighafi za kuendesha viwanda husika na yana mnyororo mpana wa uzalishaji ambao una fursa ya kutoa ajira nyingi.   

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo (Ijumaa, Septemba 15, 2017) Bungeni mjini Dodoma alipowasilisha hotuba yake ya kuahirisha Mkutano wa Nane wa Bunge. Amesema Serikali imejipanga kuimarisha usimamizi katika uzalishaji na uuzaji wa mazao hayo.

Amesema Serikali itahakikisha kuwa kila taasisi iliyopewa dhamana ya kusimamia mazao hayo, inatekeleza majukumu yake ipasavyo sambamba na kuhakikisha kwamba Watendaji wake wanafanya kazi hiyo kwa uadilifu na ufanisi mkubwa.

Amesema jitihada hizo zinalenga kuwawezesha wakulima wengi hususan wa vijijini ambao ni takriban asilimia 75 ya Watanzania wote, kulima kilimo cha kisasa, chenye tija na cha kibiashara, hivyo kuondokana na umaskini wa kipato.

“Vilevile, kuwawezesha wakulima kupata mbinu za kisasa za kuyafikia masoko ya uhakika ya mazao yao ili kupata bei nzuri ambayo itawakwamua kiuchumi. Mazao mengine ya kibiashara yatakayotiliwa mkazo ni katani, ufuta, alizeti, mbaazi na ngano.”

Amesema kwa kipindi kirefu uzalishaji wa mazao hayo ulishuka kulitokana na changamoto mbalimbali ikiwemo ya baadhi ya viongozi wa vyama vya Ushirika kushindwa kutekeleza vyema wajibu wao, wizi, dhuluma kwa wakulima na pia ushiriki mdogo wa Maofisa Kilimo katika kusimamia kilimo cha kitaalam.

Wakati huo huo, Waziri Mkuu amesema jumla ya vijana 1,000,000 wamelengwa kupata urasimishaji  ujuzi kati ya mwaka 2017 na 2021 kupitia Mpango wa Kutathmini na Kurasimisha Ujuzi uliopatikana nje ya Mfumo Rasmi wa Mafunzo.

Amesea Serikali imeamua kuchukua hatua hiyo ili kuwawezesha vijana ambao ndiyo nguvu kazi wachangie kikamilifu katika kujenga uchumi wa Taifa. “Hadi sasa tayari vijana wengi wanaendelea kunufaika na mpango huu kutoka mikoa mbalimbali.”

Miongoni mwa faida za mpango huo ni pamoja na kuwasaidia mafundi waliojifunza kupitia sehemu za kazi kupata kazi zenye staha na kuwajengea uwezo wa kushiriki na kushindana kikamilifu katika soko la ajira. Pia kuinua tija mahali pa kazi na kusaidia waajiri/wenye makampuni kukidhi viwango katika eneo la rasilimali watu. 
Waziri Mkuu amesema mpango huu unafadhiliwa kwa asilimia 100 na Serikali na unatekelezwa kwa pamoja na Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi ( VETA)

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
S. L. P. 980,
40480 - DODOMA.        
IJUMAA, SEPTEMBA 15, 2017

No comments:

Post a Comment

Pages