HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

November 16, 2017

WAZIRI MKUU AKUTANA NA MABALOZI WA TANZANIA KATIKA NCHI ZA MISRI NA ZAMBIA

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na Balozi Meja Jenerali Issa Suleiman Nassoro wa Misri  (katikati) na Balozi Abdulrahman Kaniki wa Zambia Ofisini kwake mjini Dodoma Novemba 16, 2017. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)

 
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amekutana na kufanya mazungumzo na Mabalozi wa Tanzania nchini Misri, Balozi Meja Jenerali Issa Suleiman Nassoro na Balozi Abdulrahman Kaniki wa Zambia, ambapo amewataka wakaimarishe mahusiano baina ya nchi zote mbili.

Amekutana na Mabalozi hao Balozi leo (Alhamisi, Novemba 16, 2017) katika Ofisi ya Waziri Mkuu iliyopo Barabara ya Reli na Mahakama mijini Dodoma na kuwasisitiza wakaboreshe shughuli za Kidiplomasia kati ya Tanzania na nchi za Misri na Zambia.

Pia Waziri Mkuu amewataka Mabalozi hao wakahakikishe wanatangaza vivutio vya utalii vilivyopo nchini, ukiwemo mlima Kilimanjaro, mbuga za wanyama, fukwe pamoja na fursa za uwekezaji zilizopo nchini hususan katika sekta ya viwanda.

Amesema licha ya kutangaza fursa za uwekezaji na vivutio vya utalii pamoja na kuboresha biashara baina ya Tanzania na nchi za Misri na Zambia pia wakawashawishi wawekezaji waje wawekeze katika sekta mbalimbali nchini ikiwemo ya viwanda.

Waziri Mkuu amesema Tanzania ni nchi salama yenye amani na utulivu wa kisiasa, pia Serikali imeweka mazingira mazuri ya uwekezaji jambo ambalo litawawezesha wawekezaji watakaokuja kuwekeza nchini kupata tija.

Pia Waziri Mkuu amewataka Mabalozi hao wahakikishe wanakwenda kutafuta masoko ya bidhaa mbalimbali zinazozalishwa nchini.

Hata hivyo, Waziri Mkuu amewataka Mabalozi hao kwenda kukutana na kufanya mazungumzo na Watanzania waishio kwenye nchi hizo na kuwasisitiza waishi kwa kuzingatia sheria za nchi husika. Pia wawaunganishe pamoja na kuwashauri waje kuwekeza nchini.

Kwa upande wao Mabalozi hao wamesema watahakikisha wanayafanyia kazi maelekezo yote waliyopewa na Waziri Mkuu ikiwa ni pamoja na kwenda kutafuta wawekezaji ili wawe kuwekeza katika sekta ya viwanda na kuboresha ushirikiano baina ya Tanzania na nchi hizo.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU, 
S. L. P. 980,
DODOMA.
ALHAMISI, NOVEMBA 16, 2017.

No comments:

Post a Comment

Pages