HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

December 01, 2017

INDIA KUIKOPESHA TANZANIA DOLA MILIONI 500 KUJENGA MIRADI YA MAJI KATIKA MIJI 17 NCHINI

Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dk. Philip Isdor Mpango (Mb) wa pili kulia akielezea kuhusu uwekezaji wenye kuongeza thamani ya mazao ya kilimo ambao ni fursa kwa nchi hiyo, wakati wa Mkutano na Balozi wa India nchini Tanzania Bw. Sandeep Arya (wa pili kulia), katika ukumbi wa Wizara ya Fedha na Mipango Jijini Dar es Salaam.

 
Na Benny Mwaipaja, Dar es Salaam

Serikali ya India imeahidi kutoa mkopo nafuu wa Dola za Marekani milioni 500 kwa ajili ya kutekeleza mradi mkubwa wa maji katika miji 17 nchini kupitia Benki ya Exim ya nchini humo.

Hayo yamesemwa Jijini Dar es Salaam na Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Mpango wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa India hapa nchini Bw. Sandeep Arya.

Dkt. Mpango alieleza kuwa mradi huo umelenga kumtua ndoo mama kichwani na kwamba mkopo huo utakapo patikana utasaidia kutatua kero kubwa ya maji inayoikabili jamii hivyo kuchochea kwa kasi ukuaji wa uchumi.

“Tuko katika mazungumzo ya kukamilisha upatikanaji wa mkopo huo ikiwemo kuangalia namna ya kushughulikia madai ya Benki ya Exim ambayo inataka hata kampuni itakayotekeleza mradi huo isamehewe kodi zote zikiwemo zinazopaswa kulipwa na wafanyakazi wake” alieleza Dkt. Mpango

Alibainisha kuwa licha ya kwamba jambo hilo ni gumu kisheria lakini kutokana na umuhimu wa suala hilo la maji, Serikali italipatia ufumbuzi  hivi karibuni ili mradi huo uweze kuanza mara moja.

Dkt. Mpango alitambua mchango mkubwa wa Serikali ya India katika kutatua changamoto ya maji kwa watanzania ambapo amesema kuwa inchi hiyo inatatekeleza mradi mkubwa wa maji wa Ziwa Victoria-Shinyanga hadi Tabora.

Dkt. Mpango aliiomba Serikali ya India iendelee kuisaidia Tanzania katika Nyanja za utaalamu wa teknolojia ya habari na mawasiliano-TEHAMA ili kupata watu wenye ujuzi utakao saidia  kuchochea kasi ya maendeleo ya Sekta ya Viwanda nchini.

Dkt. Mpango alisema kuwa  nchi ya India imepiga hatua kubwa katika masuala ya TEHEMA hivyo ni vema ikawekeza kwenye eneo hilo  katika Taasisi za Elimu hapa nchini ili kuweza kuwapatia ujuzi idadi kubwa ya watu watakao kwenda kusukuma gurudumu la maendeleo hasa ya ukuaji wa viwanda.

“Bila kuwa na watu wenye ujuzi katika kada mbalimbali hasa TEHAMA hatuwezi kuwa na nchi yenye uchumi wa viwanda”, aliongeza Dkt. Mpango.

Aliyataja maeneo  yenye fursa kubwa za uwekezaji kuwa ni pamoja na Sekta ya Kilimo ambapo Tanzania inahitaji kuwa na viwanda vitakavyoongeza thamani ya mazao na pia kuwa na zana bora za kilimo kama utumiaji wa Trekta badala ya kutumia jembe la mkono.

Maeneo mengine ni sekta ya utalii, afya, uendelezaji wa ujuzi kupitia fani nyeti za udaktari ama utaalamu nyeti ya tiba ikiwemo magonjwa ya moyo na figo, ambayo India imepiga hatua kubwa.

“Pia ujuzi wa Wahandisi katika Sekta ya Maji unahitajika ili kutoa huduma ya maji kwa weledi kwa jamii kwa kuwa ni moja ya hitaji muhimu kwa maendeleo, hata hivyo zipo sekta nyingine za uwekezaji kama  Utalii na  Uvuvi hasa katika kina kirefu ambao unahitaji zana bora” aliongeza Dkt. Mpango

Kwa upande wake Balozi wa India nchini Tanzania Bw. Sandeep Arya,  amesema nchi yake inania ya kuwekeza katika Kilimo, Nishati ya Umeme hasa wa Jua na kusaidia katika mpango wa ujenzi wa Mji wa Dodoma pamoja na ujenzi wa Reli na Barabara.

Amesema Tanzania na India zinauhusiano wa muda mrefu hivyo nchi yake itaendelea kuwekeza Tanzania katika Nyanja mbalimbali ili kuendeleza ushirikiano wenye tija kwa wananchi wa pande hizo mbili.

Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb), amemshukuru Balozi wa India na Nchi yake kwa nia ya kuendelea kuwekeza Tanzania na kusifu juhudi za uwekezaji mkubwa ambao unafanywa hasa katika Sekta ya Afya na kuahidi kuendelea kudumisha ushirikiano huo.

No comments:

Post a Comment

Pages