HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

January 24, 2018

ALIYEPIGA PICHA NYUFA ZA HOSTELI UDSM AOMBA ULINZI

NA JANETH JOVIN

MWANAFUNZI wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Kumbusho Dawson ambaye alitoa taarifa kuhusu hosteli mpya za chuo hicho kuwa na nyufa, amesema kwa sasa anaishi kwa hofu kutokana na kufatiliwa na watu wasiojulikana.

Dawson amesema Januari 18 mwaka huu alianza kufatiliwa na watu asiyowafahamu ambao anadai kuwa wanataka kumteka.

Akizungumza jijini Dar es Salaam, Dawson alisema tangu hali hiyo itokee amekuwa akiishi kwa hofu hali inayomfanya ashindwe kwenda sehemu yoyote.
Alisema hali hiyo imemuathiri hata kimasomo kwani kwa sasa hawezi kuhudhuria vipindi vya usiku chuoni kutokana na kuhofia kukamatwa na watu wabaya.

"Tangu tukio hilo la kutaka kukamatwa na watu nisiyowajua nimekuwa nikiishi kwa hofu na shida sana,  hali hii inanifanya nashindwa kutembea muda wote nakaa ndani au nikitaka kutoka lazima niambatane na watu watatu au wanne.

Kutokana na hali hii nashindwa kusoma vizuri nimekuwa naishi kama mkimbizi katika nchi yangu sijui hawa watu wanaonitafuta wanania gani na mimi naomba wanipe uhuru wa kukaa katika nchi yangu waniache nisome ili baadae nije kuisaidia nchi yangu,"alisema.

Aidha Dawson alisema anaviomba vyombo vya dola kumlinda kwani ameshatoa taarifa Polisi na katika vyombo vyote vya ulinzi na usalama.

"Mimi ni raia wa Tanzania na kwa mujibu wa katiba ya nchi nina haki ya kulindwa hivyo naviomba vyombo vya dola kunilinda na kuwakamata watu hao ambao ni wa halifu, "alisema.
Picha za nyufa hizo zilianza kusambaa Desemba 3 mwaka jana ambapo zilikuwa zikionyesha nyufa katika majengo hayo yaliyozinduliwa na Rais John Magufuli Aprili 15, 2017.
Ujenzi wa hosteli hizo ulifanywa na Wakala wa Majengo (TBA) kwa muda wa miezi minne na kugharimu Bilioni 10.

No comments:

Post a Comment

Pages