HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

February 19, 2018

MWILI WA KATIBU WA CHADEMA KUAGWA

Viongozi wa Chadema wakiwemo wakuu na waandamizi, wanatarajiwa kuongoza shughuli ya utoaji wa heshima za mwisho kwa mwili wa aliyekuwa Katibu wa Chama Kata ya Hananasif, Jimbo la Kinondoni, Kamanda Daniely John, itakaofanyika kesho Jumanne, Februari 20, 2018, jijini Dar es Salaam.

Mwili wa Kamanda Daniely unatarajiwa kufika nyumbani kwake Hananasif kutokea Hospitali ya Taifa Muhimbili majira ya saa 4 asubuhi kisha utapelekwa Kanisa Katoliki Hananasif (maarufu kwa Pinda) kwa ajili ya misa ya kumuombea marehemu itakayoanza saa 5 asubuhi kanisani hapo.

Baada ya ibada hiyo, waombolezaji watatoa heshima zao za mwisho kwa Kamanda Daniely kabla ya mwili wake kusafirishwa kwenda mkoani Iringa ambako atazikwa siku ya Jumatano, katika Kijiji cha Chikelewatu, wilayani Mafinga.

Itakumbukwa kuwa Kamanda Daniely alikutwa eneo la Coco beach akiwa ameuwawa kikatili na watu wanaodaiwa hawajulikani baada ya kutekwa Jumapili usiku wiki iliyopita akitokea kwenye shughuli za kampeni za uchaguzi wa marudio Jimbo la Kinondoni.

Kwa mujibu wa Reginald Malya ambaye alitekwa pamoja na marehemu Daniely kabla ya yeye kunusurika katika tukio hilo huku akiwa amejeruhiwa vibaya, amesimulia kuwa watekaji walipokuwa wakiwatesa walikuwa wakiwahoji kwanini wanajihusisha na kuipigia kampeni CHADEMA.

Hadi sasa Jeshi la Polisi halijatoa taarifa yoyote ya maendeleo ya uchunguzi wa tukio hilo la kikatili kabisa ambalo ni mwendelezo wa matukio mbalimbali ya namna hiyo yanahohusisha kupotea, kutekwa, kuteswa, kushambuliwa kwa risasi kwa ajili ya kuuwawa na kuuwawa kwa wanachama na viongozi wa CHADEMA katika maeneo mbalimbali nchini huku kukiwa hakuna uwajibikaji wowote wala hatua za kisheria katika matukio hayo na dhidi ya wahusika.

Tunatoa wito kwa wapenzi, wanachama, viongozi wa CHADEMA na Watanzania wote wenye mapenzi  mema kwa nchi yao wanaoguswa na hali tete ya usalama wa raia na mali zao ndani ya nchi kwa sasa, kujitokeza kutoa heshima zao za mwisho kwa Ndugu Daniely John hapo kesho.

Imetolewa leo Februari 19, 2018 na;

Tumaini Makene
Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano

No comments:

Post a Comment

Pages