HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

December 13, 2018

NGORONGORO NATIONAL OPEN CHAMPIONSHIP KUUNGURUMA ARUSHA

Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Riadha Tanzania (RT), Tullo Chambo, akizungumza na waandishi habari jijini Arusha kuhusu Mashindano Wazi ya Taifa ya mchezo wa riadha 'Ngorongoro National Open Championship,' yatakayofanyika jijini Arusha.





NA MWANDISHI WETU

WASHINDI wa Mashindano Wazi ya Taifa ya mchezo wa riadha 'Ngorongoro National Open Championship,' wanatarajia kutembelea Hifadhi ya Taifa ya Ngorongoro, kama moja ya zawadi ya wale watakaofanya vizuri Desemba 14 jijini Arusha.

Hayo yalisemwa na Katibu wa Shirikisho la Riadha Tanzania (RT), Wilhelm Gidabuday, wakati akizungumza na gazeti hili kuhusiana na mashindano hayo yaliyopangwa kuanza jijini Arusha katika viwanja vya Sheikh Amri Abeid.

Gidabuday alisema katika mashindano hayo washindi wa mbio hizo, mbali na zawadi zilizopangwa wao watakwenda kutembelea mbuga hizo kama moja ya vivutio kutoka kwa wadhamini wa mashindano hayo.

Alisema kutokana na hilo wanariadha wanapaswa kuongeza bidii katika mazoezi ambayo wanafanya kwa ajili ya kujiandaa na mashindano hayo.

"Tumefurahi sana kupata udhamini kutoka Ngorongoro tuna imani mashindano yatafana," alisema Gidabuday.
Alisema mashindano hayo ni muhimu kwa wanariadha kuonyesha viwango vyao, jambo litakaloiwezesha Kamati ya Ufundi ya RT kuwa na ‘base’ ya wachezaji walioko kwenye viwango hivi sasa.

Alisema mwaka uliopita kutokana na kutekeleza kalenda ya RT, hawakuwa na mashindano ya Taifa, hivyo wameona ni lazima mwaka huu vijana wakapata nafasi muhimu kuonyesha viwango vyao jambo litakalosaidia kuchagua timu ya Taifa.

Alisema kuwa, washindi watakaofanya vizuri zaidi watapata fursa ya kushiriki mashindano mbalimbali ndani na nje ya nchi ikiwemo Japan, kusaka viwango vya kufuzu mashindano ya kimataifa ikiwamo World Championship na Olimpiki.
Awali, RT ilipanga mashindano ya taifa kufanyika kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, Novemba 16 kabla ya kuahirishwa.

Gidabuday aliitaja michezo itakayoshindaniwa kuwa ni Mita 100, Relay 100x4, 200, 400, Relay 400x4, 800, 1,500, 5,000 na Mita 10,000, na KM 10,Kuruka Juu, Kuruka Chini, Miruko Mitatu, Kurusha Mkuki, Tufe na Kisahani kwa wanaume na wanawake.

Alisema kutakuwa na zawadi kwa washindi, ambapo mshindi wa kwanza atapata Medali ya Dhahabu na Sh. 150,000, wa pili Medali ya Fedha na Sh. 100,000, huku wa tatu akiondoka na Medali ya Shaba na Sh. 50,000.

Aidha, alitoa wito kwa wadau wengine kuzidi kuiunga mkono Riadha Tanzania kama ambavyo wanavyofanya Ngorongoro.

No comments:

Post a Comment

Pages