HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

January 17, 2019

KAMATI YA BUNGE YAISHAURI SERIKALI IMALIZIE MAZUNGUMZO YA SHILINGI BIL.345 ZA UTALII KUSINI

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge Ardhi, Maliasili na Utalii, Nape Nnauye ( wa tatu kushoto) akiwa na Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt.Hamis Kigwangalla pamoja na wajumbe wa kamati hiyo wakipewa maelezo na Mkuu wa Hifadhi ya Taifa ya Mikumi, Godwell Meing'ataki kuhusiana na bwawa  lenye viboko wengi katika Hifadhi hiyo liitwalo Mwanambogo wakati wajumbe ya Kamati hiyo walipofanya ziara ya kutembelea kwa ajili ya kujionea mradi wa kukuza utalii kusini wa Regrow ulipofikia na namna unavyotekelezwa.Wa kwanza kushoto ni Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Constantine Kanyasu. (Picha na Lusungu Helela)


Kamati ya Kudumu ya Bunge  Ardhi, Maliasili na Utalii imeishauri Serikali imalize mazungumzo na Benki ya Dunia juu ya hatma ya mkopo wa mradi wa kukuza utalii kwa upande wa kusini baada ya Benki hiyo kuonesha kusuasua kufuatia Serikali ya Tanzania kusimamia uamuzi wake wa kuanzisha Mradi wa kufua umeme wa Mto Rufiji.

Hatua hiyo inakuja baada ya serikali ya Tanzania kukopa jumla shilingi bilioni 345 kutoka Benki ya Dunia ili kukuza utalii katika maeneo ya Kusini kupitia mradi ujulikanao kama Resilient Natural Resource Management for Tourism Growth ( REGROW)

Hayo yamebainishwa na Mwenyekiti Kamati hiyo, Mhe .Nape Nnauye baada ya Kamati hiyo  kufanya ziara katika Hifadhi ya Taifa ya Mikumi ikiwa ni moja ya ziara ya  kutembelea ukanda wa kusini kwa ajili ya kuona mkopo huo umefikia wapi na namna mradi huo unavyotekelezwa.

Amesema uamuzi huo  wa Serikali wa kutaka kufungua Utalii wa Kusini ni wa muhimu sana hata endapo mazungumzo hayo yanayoendelea yatakwama Serikali ifikirie mbadala wake lengo likiwa ni kuongeza mapato yatokanayo na utalii.

Katika mradi huo Hifadhi za  Mikumi, Ruaha, Udzungwa pamoja na Pori la Akiba la Selous zinatarajiwa kunufaika kupitia mkopo huo  lengo likiwa ni kufanya ukanda wa kusini kuwa lango la Utalii kama ilivyo kwa ukanda wa kaskazini.

Katika hatua nyingine, Mwenyekiti huyo ameishauri Serikali kuwa endapo fedha za  mkopo huo zitapatikana iandae utaratibu wa kuufanya mradi huo uwe wa kibiashara badala ya ilivyo sasa ambapo kwa kiasi kikubwa matumizi ya fedha hizo yamejikita katika uhifadhi zaidi.

Amesema fedha  inayowekezwa ni  nyingi na italipwa na watanzania sasa ni vizuri itakapowekezwa itoe matokeo yaliyokusudiwa ambayo yatafanana na thamani ya mkopo wenyewe.

Kwa upande wake, Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt.Hamis Kigwangalla amesema kumekuwa na mashaka kidogo kutoka kwa Wafadhili ambao wanatukopesha  pesa hizo baada ya kuona  mradi wa kufua umeme katika mto Rufiji unatekelezwa.

Amefafanua kuwa Wafadhili hao wanahofu kuwa kutakuwa na uharibifu mkubwa wa mazingira na hivyo mradi wa Regrow utashindwa kutekelezwa kwa vile  kivutio katika Pori la Akiba la Selous kitabadilika sura yake

Ameelezea kuwa  Serikali imefanya  jitihada za kuhakikisha kuwa  mazingira ndani ya Pori hilo hayataharibiwi na hivyo mradi wa Regrow unaweza ukaendelea kama ilivyopangwa.

Amesema moja ya hatua zilizochukuliwa na serikali ni kuvihamisha viumbe ambavyo vilikuwepo  katika eneo linapotarajiwa bwawa kujengwa, Hivyo viumbe hao wataendelea kuwepo na wanaweza kurudi katika eneo lao la awali.

Aidha,Mhe.Kigwangalla amesema hata kama itatokea viumbe hao wakapotea kutokana na ujenzi wa bwawa hilo basi viumbe na mimea iliyokuwepo katika eneo hilo vitarudishiwa kwa sababu tayari imechukuliwa na kuhifadhiwa kwenye maabara ya vyuo vikuu mbalimbali vilivyopo hapa nchini kikiwemo  Chuo kikuu Cha Dar es Salaam pamoja na Sokoine.

"Tumewaeleza kuwa mashaka yao hayawezi kuzuia huu mradi na bila shaka wametuelewa hivyo tunasubilia uamuzi wa mwisho wa kuamua wanatukopesha au hawatukopeshi" amesema Mhe. Kigwangalla.

Pia amesema katika mradi huo yatachimbwa mabwawa makubwa  matatu ambayo yatatumika kama vyanzo vya maji kwa wanyama waliopo katika bonde la Mto Rufiji


Akizungumzia manufaa ya mkopo huo , Waziri Kigwangalla amesema utatumika kujenga miundombinu mbalimbali  ikiwemo barabara pamoja na viwanja vya ndege ambavyo vitakuwa vichocheo vikubwa katika kukuza na kuendekeza utalii kwa ukanda wa kusini.

No comments:

Post a Comment

Pages