HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

February 20, 2020

BILIONI 8.8 ZIMETUMIKA KUJENGA HOSPITALI NA VITUO VYA AFYA MKOANI TABORA

NA, TIGANYA VINCENT, TABORA

SERIKALI imetoa jumla ya shilingi bilioni 8.8 kwa  Mkoa wa Tabora kwa ajili ya kukarabati na kujenga Hospitali na Vituo vya Afya katika kipindi cha 2015 hadi Desemba 2019 ili kusogeza huduma za utoaji wa tiba kwa wananchi.

Hatua hiyo imeondoa adha kwa wananchi kutembea umbali mrefu kutafuta huduma za afya na kurahisi upatikanaji wa vifaa tiba na huduma za upasuaji katika maeneo yaliyo karibu na wanapoishi.

Kauli hiyo imetolewa jana na Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri alipokuwa akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa ilani ya Uchaguzi wa Chama cha Mapinduzi (CCM) kwa Wajumbe wa Kamati ya Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa wa Tabora.

Alisema kati ya fedha hizo shilingi bilioni 3 zimetumika kujenga Hospitali za Wilaya ya Sikonge na Uyui  ambapo ujenzi umekamilika kwa asilimia 97.
Mwanri alisema kuwa shilingi bilioni 1 zilitumika katika kukarabati Vituo vya Afya vya Zogolo cha Halmashauri ya Nzega Mji, na Upuge cha wilaya ya Uyui.

Alisema kuwa shilingi bilioni 4.8 zimetumika katika ujenzi na ukarabari wa Vituo vya Afya vya Simbo cha Igunga, Ulyankulu cha Kaliua , Ussoke cha Urambo, Kitunda na Kipili vya Sikonge, Busondo cha Nzega na Ussoke Mlimani cha Urambo.

Mwanri aliongeza kuwa vituo vingine ni Igurubi cha Igunga, Maili Tano kilichopo Manispaa ya Tabora, Igalula cha Wilayani Uyui na ujenzi wa Wodi ya Mama na Mtoto katika Hospitali ya Wilaya ya Nzega.

Naye Katibu Mwenezi wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Urambo Obed Balola alizitaka Halmashauri ya Wilaya ya mbalimbali kuongeza juhudi kuandika wananchi wanaojiunga na Mfuko Afya ya Jamii(CHF) ili waweze kupata huduma za afya kwa gharama nafuu.

Alisema Mkoa wa Tabora una ya Kaya 421,023 ambapo hadi hivi sasa kuna kaya 5,780 ambapo ni wananchi 29,713 ndio wananufaika na huduma hiyo.

Balola alisema idadi hiyo ni kidogo jambo ambalo linaonyesha kuwa watu wengi bado hawana uhakika na huduma za afya.

Kwa upande wa Mbunge wa Jimbo la Manonga Seif Gulamali ameipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa kutoa fedha nyingi kwa ajili ya miradi mbalimbali ikiwemo ya afya.

No comments:

Post a Comment

Pages