NA VICTOR MASANGU, PWANI
SERIKALI mkoani Pwani imesema kwamba imeridhishwa na mwenendo wa utekelezaji wa miradi mbali mbali ya maji ambayo inasimamiwa na Ruwasa kwa kutekeleza miradi ipatayo 26 katika maeneo ya vijijini ambayo imegharimu kiasi cha shiingi bilioni 3.9 kwa lengo la kuwaondolewa wananchi changamoto ya kutembea umbari mrefu kwa ajili ya kutafuta maji.
Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Pwani Mhandisi Evarist Ndikilo wakati alipokuwa akizungumza katika kikao cha wadau wa Sekta ya maji Vijijini katika Mkoa huo kilichoandaliwa na Wakala wa maji na usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) na kuhudhuliwa na viongozi mbali mbali wa serikali wenyeviti wa halmashauri pamoja na wabunge kutoka majimbo mbali mbali ya Mkoa huo.
Pia Ndikilo alibainisha kwamba suala la ulipaji wa bili za maji katika Mkoa huo bado ni tatizo hali inayosababisha baadhi ya maeneo ya baadhi ya miradi ya maji kufa na kusababisha ukosefu wa huduma hiyo.
Injinai Ndikilo alisema kuwa katika Wilaya ya Rufiji na Wilaya ya Kibaha Vijijini ipo miradi ya maji lakini kutokana na baadhi ya watu kutokuwa na tabia ya kutolipa bila kwa wakati inapelekea miradi hiyo kufa na kupelekea baadhi ya maeneo kukosa maji kabisa na wananchi kuanza kusumbuka kutafuta maji katika maeneo mengine..
"Suala la ulipaji wa kodi wa bili za maji katika Mkoa wetu wa Pwani bado ni tatizo, wananchi wanafikiri huduma ya maji ni bure, kama kuna eneo tunafeli basi ni hili tunatakiwa kutambua kuwa maji ni bidhaa kama ilivyo bidhaa nyingine tulipie ili tuendelee kunufaika nayo" alisema.
Ndikilo alisema wananchi na Taasisi wanatakiwa kulipa bili za maji kwa wakati ili huduma iwe endelevu na inapotokea hawalipi inasababisha kukwama kwa miradi hiyo na kukosa nguvu ya kujiendesha.
Aidha alisema suala la ulinzi wa vyanzo vya maji ni jukumu la kila mmoja hivyo isiachiwe Ruwasa pekee kwani wanufaika ni wananchi ambao baadhi yao wanaishi karibu na vyanzo hivyo.
Aliwaagiza Wakurugenzi wa Halmashauri za Mkoa huo pamoja na wenyenyeviti wa Halmashauri kutumia mabaraza ya Madiwani kujadili suala la kutenga maeneo kwa ajili ya ujenzi wa ofisi za Ruwasa ili kuwaondolea kero iliyopo sasa.
Katika hatua nyingine ameziagiza Ruwasa, Dawasa na Eura kukutana kwa pamoja kujadili namna ya kutatua kero za bili za maji ambazo zimekuwa zikilalamikiwa na wananchi.
Meneja wa Ruwasa Mkoa wa Pwani Beatrice Kasimbazi alisema hadi kufikia Desemba 2020 asilimia 73 ya wakazi waishio Vijijini wanapata maji kwa asilimia 71 huku maeneo ya Mjini wakipata asilimia 84.
Kasimbazi alisema kwa kipindi Cha kuanzia 2019 hadi Februari 2021 miradi 48 yenye gharama ya zaidi ya Shilingi Biln 9.8 inaendelea na utekelezaji ambayo itanufaisha wakazi 99,334.
Meneja huyo alisema katika mwaka 2021/2022 Mkoa umejipanga kutekeleza miradi 65 itakayogharimu Shilingi 18.7.
Mkuu wa Wilaya ya Rufiji Luteni Kanal Patrick Sawala malalamiko kutoka kwa baadhi ya wananchi wake Wilaya hiyo ni bili kubwa za maji kuliko uhalisia wa matumizi.
Sawala ameomba usomaji wa bili za maji uangaliwe upya ili kuondoa kero za mara kwa mara zinazosababisha kuwepo kwa ugumi wa wananchi kulipa bili.
Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kisarawe, Mussa Gama ameiomba uongozi wa Ruwasa kuhakikisha kwamba wanapeleka huduma ya maji katika vijiji mbali mbali kwa lengo ka kuweza kuwaondolea changamoto ya wananchi kutembea umbari mrefu kwa ajili ya kutafuta maji.
“Kwa upande wangu mimi nizungumzie suala la changamoto katika baadhi ya maeneo mbali mbali ya vijijini ambavyo vipo katika halmashauri ya Kisarawe na sisi tuna mradi mkubwa wa maji ambao ulizinduliwa na Rais Dk John Pombe Magufuli hivyo ni vema wenzetu wa Ruwasa wakaweka mikakati ya kuwasambazia maji wananchi wetu,”alisema Gama.
No comments:
Post a Comment