HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

July 15, 2018

WAZIRI MKUU AKEMEA MAHUSIANO MABAYA YA WATUMISHI KAHAMA

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, akisalimiana na aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Fadhili Nkulru wakati alipowasili kwenye viwanja vya ukumbi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kahama  kuzungumza na watumishi wa Umma. Hii ilikuwa jana Julai 14 na leo Julai 15 Rais John Magufuli ametengua uteuzi wake. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amekemea mahusiano mabaya baina ya watumishi wa wilaya ya Kahama na kusema wanapaswa kubadilika mara moja.

Ametoa onyo hilo leo (Jumapili, Julai 15, 2018) wakati akizungumza na watumishi na viongozi wa Halmashauri za Wilaya za Ushetu, Msalala na Kahama Mji, wilayani Kahama mkoani Shinyanga.

“Hali ya mahusiano hapa Kahama ni mbaya kuliko Kishapu na Shinyanga. Mnachapa kazi vizuri lakini tatizo kubwa kila mmoja anaenda kivyake, hakuna anayemsikiliza Mkurugenzi wa Halmashauri wala Mkuu wake wa idara,” amesema.

Waziri Mkuu ambaye yuko kwenye ziara ya siku tano ya kikazi mkoani humo, amewaeleza watumishi na viongozi hao kwamba Serikali haitavumilia kuona watumishi wa aina hiyo wanaendelea kufanya kazi.

“Serikali haitavumilia kuona watumishi wakifanya mambo ya hovyo. Kahama ni wilaya yenye majaribu na Shinyanga nayo ni wilaya yenye majaribu makubwa. Kwa hiyo watumishi inabidi muwe makini, kuweni waangalifu msije mkaingia kichwakichwa kwenye majaribu haya.”

“Migogoro niliyoisikia ambayo iko hapa ni kwa sababu ninyi mmeingia kwenye biashara na kutake sides. Hapa Kahama, Mkuu wa Wilaya na Mkurugenzi wa Wilaya hamuelewani, Mkurugenzi na wakuu wa idara hamuelewani, wakuu wa idara na wasaidizi wao nao pia hawaelewani,” alisema.

“Napenda kusisitiza kwamba ninyio ni viongozi wa umma, kwa hiyo ni lazima mzingatie itifaki za kiuongozi, mzingatie mahusiano mema mahali pa kazi. Hatupendi viongozi muwe chanzo cha matatizo hapa Kahama,” aliwaasa.

Alisema Kahama ina fursa kubwa na nzuri kwenye kilimo, madini, mifugo na biashara na akawataka viongozi wanaoletwa kwenye wilaya hiyo wawe makini. “Kiongozi ukiletwa hapa inabidi uwe na kichwa kilichotulia. Inabidi uwe mwaminifu sana ili uweze kudumu kwenye wilaya kama hii,” alisisitiza.

“Kama kiongozi ulizoea kwenda disco inabidi uache, kama ulizoea kwenda baa inabidi ununue kreti uweke ndani kwako. Kama ulizoea kushabikia mpira kwa kujichora chaki, sasa basi. Kaa sebuleni kwako, angalia mpira kwenye luninga yako, ndiyo dhamana ya uongozi hiyo,” alisema.

Aliwataka watumishi wa umma wawasaidie wananchi kuboresha utendaji wao kwenye kilimo, uvuvi na ufugaji ili kila kuleta tija kwenye kila sekta.

Waziri Mkuu leo anaendelea na ziara yake wilayani Kahama kwa kukagua shughuli za maendeleo na kuzungumza na wananchi.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMAPILI, JULAI 15, 2018.

No comments:

Post a Comment

Pages