November 02, 2022

Rais Samia aagiza kuundwa Kikosi Kazi kushughulikia Nishati Safi ya Kupikia

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan akihutubia Viongozi pamoja na Wananchi waliohudhuria kwenye Kongamano la Kitaifa kuhusu Nishati Safi ya Kupikia katika Ukumbi wa Julius Nyerere (JNICC).
Rais Samia akiwa na viongozi.
 

 
Na Hussein Ndubikile, Dar es Salaam

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan ameelekeza kuundwa kwa Kikosi Kazi kitakacho shughulikia Nishati Safi ya kupikia nchini lengo likiwa kulitoa Taifa kwenye matumizi ya nishati zisizofaa.

Kauli hiyo ameitoa leo jijini Dar es salaam wakati akifungua kongamano la la Kitaifa kuhusu Nishati Safi ya Kupikia katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Mwalimu Julius Nyerere(JNICC).

Amesema kuwa kikosi kazi hicho hakitakuwa cha Serikali pekee, bali kitahusisha pia sekta binafsi na wadau wa maendeleo na kitakuwa na kazi ya kuchambua sera za Serikali pamoja na mapendekezo ya wadau.

Amebainisha kuwa kikosi kazi hicho kitaongozwa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kwa ngazi ya mawaziri na uratibu zote zitafanyika chini ya Wizara ya Nishati.

"Kikosi kazi hicho kitakuja na mpango mkakati ambao utaiongoza Serikali, sekta binafsi na wadau wa maendeleo kutafuta suluhu ya nishati safi na endelevu ya kupikia" Alisema rais Samia.

Amesisitiza kuwa kwa mujibu takwimu zilizopo kaya zinazopikia kwa kutumia mitungi ya gesi ni asilimia 5, umeme asilimia 3 na nishati nyingine safi asilimia 2.2.

Hivyo bado kuna kazi ya kubwa ya kuhamasisha matumizi ya nishati iliyo safi na salama na pia tunapaswa kuwa na mkakati madhubuti wa kisera na kibajeti pamoja na kuweka mazingira wezeshi katika kutatua changamoto za upatikanaji wa nishati safi.

“Serikali peke yetu hatuwezi tunapaswa kwenda sambamba na sekta binafsi, nashukuru baadhi yao wameanza kujitokeza kushirikiana nao sambamba lakini si kisera kutokana kuwa ni fursa ya biashara hivyo kuna haja ya kuwa na sera inayoshughulikia suala hili,” Amesema Rais Samia

Katika hatua nyingine,Rais Samia amesema kuanzia bajeti ijayo, Serikali itatenga fedha za kutosha zitakazoanzisha mfuko wa nishati safi ya kupikia lengo ni kwenda kumtua mama mzigo wa kuni kichwani.

Awali Profesa, Anna Tibaijuka ameishauri Serikali kuweka utaratibu mzuri wa kibiashara kwa wauzaji wa nishati ya gesi  ili waweze kuyafikia maeneo mengi hasa ya vijijini. 

Amesema kuwa sehemu kubwa ya wananchi wa Vijijini wamekuwa wakikumbana na adha ya utafutaji wa kuni kwa ajili ya kupikia kitu ambacho kimekuwa kikiwapotezea muda mwingi wa kufanya shughuli za kuinua vipato vyao na hivyo kushindwa kumudu gharama za maisha.

“Mimi mwenyewe ni muhanga wa watu walikuwa wakikumbana na adha ya utafutaji kuni hivyo naelewa fika suala hili kama kweli mjadala huu unalenga kuleta unafuu ni wazi kwamba tunahitajika kuchukua hatua rafiki kwa kuwashirikisha Wafanyabiashara wa gesi,”amefafanua Tibaijuka.

Hata hivyo ameshauri Serikali pia kuangalia gharama za upandaji wa vitu mbalimbali na kuziweka katika hali rafiki kwa kila nyanja ili kuepuka kuleta nafuu ya jambo moja huku mengine yakiendelea kuwakandamiza wananchi.

Kwa upande wake, Waziri wa Nishati, January, amesema kongamano hilo linalenga kuwaokoa maelefu ya Watanzania ambao wamekuwa wakiathirika kutokana na kutumia nishati inayotokana na kuni, mkaa na mabaki ya mazao na vinyesi vya wanyama.

Takwimu zinaonyesha kuwa, zaidi ya watu 30,000 wanapoteza maisha kila mwaka kutokana na kutumia nishati ya kuni na mkaa ambayo, kiafya sio salama lakini kutokana na changamoto mbalimbali imewalazimu kutumia.


No comments:

Post a Comment

Pages