November 22, 2025

CCM yataka 'OMO' aachane na stori za Uchaguzi uliopita

Na Mwandishi  Wetu, Zanzibar 


Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimemtaka aliyekuwa Mgombea Urais  wa Zanzibar  kupitia ACT Wazalendo, Othman Masoud Othman 'OMO', iwapo  chama chake kina ubavu wa kushindana na CCM kisubiri Uchaguzi Mkuu ujao  mwaka 2030.



Pia CCM  kimeyaita madai ya kutaka Uchaguzi Mkuu  wa Zanzibar  urudiwe huku OMO akiamini  atamshinda Rais Dkt. Hussein Ali Mwimyi alisema hizo ni mbwembwe na maneno ya kujifariji kwa wafuasi wake.


Katibu wa Kamati  Maalum ya NEC  Zanziabr Idara  ya Itikadi Uenezi na Mafunzo Khamis  Mbeto  Khamis amesema hayo huku akimtaka OMO aachane na  stori za Uchaguzi kwa kuwa ukurasa huo umeshafungwa rasmi.


Mbeto  alisema inashangaza  kukisikia ACT kikidai  kuwa kilishinda wakati wananchi wameshampigia kura Rais Dkt. Mwinyi ambaye  sasa anaiongoza Serikali ya Mapinduzi na kujipanga kuendeleza maendeleo yanayoonekana.


"Mwambieni OMO aache porojo badala yake aende Ikulu akaape kuwa Makamu wa Kwanza  wa Rais Zanzibari ikiwa ameshindwa kazi awapishe wenzake washirikiane na Rais Dkt. Mwinyi  kuiletea maendeleo  Zanzibar " alisema Mbeto. 


Katibu huyo Mwenezi aliongeza kusema ACT kiache kuidanganya dunia badala yake kikubali ukweli  nguvu  za ushindi wa CCM  zimetokana na haiba  ya ustawi wa Maendeleo  yanayoonekana hivi sasa Unguja na Pemba. 


"Ile zama ya  kusambaza propaganda  uchwara kupitia  radio vifua na watu kuwadanganya vibarazani  imepita. Wananchi hawataki kushabikia siasa za chuki na migawanyiko" alisema.


Mbeto alibainisha madai kuwa uchaguzi ukirudiwa tena Rais Dk Mwimyi hatapata  kura asilimia 30, Mbeto ameyaita hayo  ni maneno yasioingia akilini na kuaminika. 


Alieleza kuwa kwa wakati  huu  hadithi za uchaguzi mkuu hazina nafasi hata ya kusikilizwa au kufuatiliwa na wananchi,  badala yake watu wanaitarajia SMZ  izidi kuongeza kasi ya mabadiliko kiuchumi, kisiasa na kijamii.


"Uchaguzi wa Mwaka 1995 wapo waliodai  Dkt. Salmi Amour ataondoshwa  kabla ya mwaka 2000. Wakasema tena Dkt. Amani Karume hamalizi muda wake. Walipokataa kushirikiana na Dkt. Ali Mohamed  Shein Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK), iliundwa na kusongambele " alisema mwenezi  huyo.

No comments:

Post a Comment

Pages