April 23, 2016

Tanesco yaichapa UDOM 3-1

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

TIMU ya soka ya Tanesco imeendeleza wimbi la ushindi kwa kuwachapa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) kwa magoli 3-1 katika mchezo uliofanyika jana asubuhi kwenye uwanja wa Jamhuri mkoani hapa.

UDOM ndio walikuwa wa kwanza kupata bao katika dakika ya kwanza ya mchezo lililofungwa na Ally Lutavi, na dakika moja baadaye Tanesco walisawazisha kwa njia ya penati kupitia Said Kondo baada ya mchezaji wao kuangushwa katika eneo la hatari.

Mchezaji Khalifa Shekuwe aliiongezea Tanesco bao la pili katika dakika ya 35 na Joseph Mzee alipigilia msumari wa mwisho kwa kuandika bao la tatu katika dakika ya 81, ambapo sasa Tanesco wamefikisha pointi saba.

Katika mchezo mwingine uliochezwa pia kwenye uwanja huo, timu ya Geita Gold Mine (GGM) waliwafunga CDA Dodoma ‘Watoto wa nyumbani’ kwa magoli 2-0.

Mabao ya GGM yalifungwa na Gwetu Guvete dakika ya 11 na Oscar Binamungu katika dakika ya 13.

Kwa upande wa  mchezo wa netiboli, timu ya Tamisemi inayoundwa na wachezaji wakongwe na wenye uzoefu waliifundisha TPDC kwa kuwafunga  magoli 40-6. Hadi mapumziko Tamisemi waklikuwa mbele kwa magoli 18-5.

Katika mchezo wa kuvuta kamba wanaume, TPDC waliwafuta machozi dada zao wa netiboli baada ya kuwavuta bila huruma Tanesco kwa 2-0.

Michuzno hiyo iliendelea baadaye jioni (jana) kwa mechi za mchezo wa netiboli za Uchukuzi SC kucheza na Tanesco, huku TPDC wakiwakaribisha CDA Dodoma, wakati kwa upande wa soka Uchukuzi SC watacheza na GGM, ambao walichelewa kufika na sasa wanacheza mfululizo.

No comments:

Post a Comment

Pages