NA MWANDISHI WETU
KLABU ya Lions Kimataifa imetoa wito kwa Olipiki Maalum
Tanzania (SOT) na kueleza kwamba
wamegundua eneo la michezo ya walemavu
wa akili ni sehemu kusaidiwa kwa hali na mali na kuahidi kuendelea kuisaidia
katika maendeleo yao.
Akizungumza jana katika ufunguzi wa michezo hiyo, hafla
iliyofanyika Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, mwakilishi wa klabu ya Lions,
Bakari Omari alisema baada ya kutafakari kwa kina wamegundua kwamba ni jukumu
lao la moja kwa moja kuwasaidia walemavu wa akili katika michezo ili kuwasaidia
kuondokana na unyanyapaa.
Omari alisema awali kabla ya kujitosa kusaidia walemavu hao waliketi na kupitia historia ya michezo yao na
kugundua kwamba inahitaji msaada zaidi kwa sababu ni eneo ambalo changamoto
zake zinahitaji wadau ambao ndio kimbilio lao.
Mkurugenzi wa mipango na Maendeleo wa Olimpiki Maalum
Afrika, Joe Mutue alitumia fursa hiyo kuishukuru Klabu ya Lions Kimataifa kwa
kusaidia kuwashirikisha walemavu wa akili kutoka kambi ya wakimbizi wa
Nyarugusu mkoani Kigoma ambao awali walitakiwa kushiriki michezo ya Taifa
iliyofanyika Zanzibar kuanzia Desemba 7-10 kwenye uwanja wa Amaan, ambao hawakushiriki kwa
sababu ya kukosa ruhusa ya ushiriki wa michezo hiyo.
Mutue alisema Lions Club kabla ya kufanikisha safari ya
wanamichezo hao 60 kutoka Nyarugusu
ambao watashiriki michezo na wengine 60 wa Wilaya za Ilala, Temeke na
Kinondoni ambao watachuana katika michezo ya soka na riadha.
Mutue alisema kupitia michezo hiyo anawaomba wanamichezo
kucheza kiungwana ili kupatikana wanamichezo ambao watashiriki michezo ya dunia
mwakani Abu Dhabi Falme za Kiarabu.
Kaimu Mwenyekiti wa
Olimpiki Maalum, Lightness Mbilla alisema mwaka 2018 umeanza vizuri kwa sababu
ya ujio wa viongozi wakubwa wa Kamati hiyo na kueleza kwamba anaona Baraka za Mungu
katika siku za usoni katika michezo ya walemavu wa akili.
Mbilla alitumia fursa hiyo kuwashukuru Lions Club kwa
mchango wao wa kuwasaidia wakimbizi kushiriki katika michezo hiyo ambako pia
wasaidie maandalizi ya michezo ya dunia ambayo Tanzania inatarajia kuwakilishwa
na wanamichezo 40.
Mbilla alisema pamoja na mchango wa Lions Club lakini wadau
wengine wamejificha na kutoipa kipaumbele michezo hiyo ambayo wanamichezo wake huleta medali nyingi
tofauti na michezo mingine.
Aidha Mbilla alitumia fursa hiyo kuiomba serikali kuwa na
jicho la tatu kusaidia michezo ya walemavu wa akili ambao wanatakiwa kuwa na
michezo mbalimbali ambayo itawasaidia wanamichezo hayo.
Kabla ya michezo hiyo kuanza, yalifanyika matukio kama kuwasha
na kukimbiza mwenge wa Kamati hiyo pamoja na kupandisha bendera yake ambayo ni
kiashiria cha ufunguzi wa michezo hiyo inayotarajia kuendelea kesho uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
No comments:
Post a Comment