HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

July 16, 2018

WAZIRI MKUU AMWAGIZA RPC SHINYANGA AWAKAMATE VIONGOZI TISA WA AMCOS YA USHETU

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akihutubia mkutano wa hadhara katika kijiji cha Kangeme  kwenye  Halmashauri ya Ushetu mkoani Shinyanga,  Julai 16, 2018. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).

*Ni kwa upotevu wa dola za Marekani 21,000
*Wakimbia mkutano baada ya wananchi kuzomea
  
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amemwagiza Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Simon Haule awakamate viongozi wa Chama cha Msingi cha Mkombozi kwa upotevu wa dola za marekani 21,000 za chama hicho.

"Wabebe hawa watu, wahoji waseme hiyo fedha iko wapi na jambo la kwanza wailete hiyo fedha ya wakulima. Wakishindwa kurejesha fedha, wawekwe ndani," amesema.

Waziri Mkuu ametoa agizo hilo leo (Jumatatu, Julai 16, 2018) wakati akizungumza na mamia ya wananchi wa kijiji cha Kangeme, kata ya Ulowa katika Halmashauri ya Ushetu wilayani Kahama ambao alienda kuzindua mpango wa Ushirika Afya na NHIF.

Waziri Mkuu amefikia uamuzi huo baada ya kuwaita viongozi wa chama cha Mkombozi watoke hadharani na kubaini kuwa hakuwepo hata mmoja. Inadaiwa kwamba walitoroka baada ya wananchi kuanza kuzomea.

Kamanda Haule amewataja watuhumiwa hao kuwa ni Mwenyekiti, Bw. Shilinde Abdallah na mhasibu wa AMCOS hiyo, Bw. Kulwa Shinzi pamoja na wajumbe saba wa bodi ya chama hicho.

Akiwa katika tukio hilo, Mwenyekiti wa Chama Kikuu cha Ushirika cha Kahama (KACU), Bw. Emmanuel Cherehani alisoma taarifa ya Chama na alipotaja bei ya tumbaku kuwa ni nzuri, wananchi walimzomea kupinga kile alichokisema. Bw. Cherehani alikuwa akitoa mafanikio ya chama hicho, na kusema kuwa bei ya tumbaku ni nzuri.

Akitoa ufafanuzi kuhusu kadhia hiyo, Waziri wa Kilimo, Dk. Charles Tizeba alisema kuna tatizo katika uteuzi (grading) wa tumbaku kwani wakulima wanalima tumbaku nzuri lakini katika upangaji bei, wanalipwa bei ndogo. “Kuna wakulima wanakidai chama cha Mkombozi kiasi cha dola za Marekani ambayo ni madai ya tumbaku waliyoiuza tangu mwaka 2014.”

Akizungumza na wananchi hao, Waziri Mkuu alisema Serikali imeamua kufufua ushirika kwa sababu ndiyo mkombozi wa wakulima. "Tumeamua kurudisha ushirika aminifu kwa wakulima, na nirudie kutoa onyo kwa viongozi waliopata dhamana ya kuongoza ushirika wasidhani kule wameenda kupata ulaji.”

“Tunataka ushirika unaosimamiwa na viongozi waaminifu. Kwenye ushirika kuna fedha na kuna mali za chama, kwa hiyo ni lazima tupate viongozi ambao ni waaminifu,” amesema.

“Kwa mfano, hapa Ulowa wakulima wamekuwa wakilalamikia kupewa bei ya chini wakati wakati wao viongozi wanabeba kile cha juu na kuwaumiza wakulima. Kiongozi wa KACU kasoma taarifa hapa mkaanza kuzomea, hiyo ni dalili tosha kwamba kuna tatizo la msingi,” amesema.

Waziri Mkuu alitumia fursa hiyo kuwaasa wakulima waachane na tabia ya kukopa pembejeo na kufunga mikataba na makampuni ya ununuzi wa tumbaku na badala yake wajiwekee akiba ili msimu wa kilimo ukianza wasirudie tena kukopa.

“Gharama za kulima ekari moja, kuweka dawa, palizi na kuchoma haizidi sh. 150,000. Wewe amua unataka kulima ekari ngapi, weka fedha zako kwenye akaunti usubiri msimu ujao. Kwenye hii biashara ya tumbaku, ukitafuta mikopo utabakia kuwa maskini kwa sababu huna nguvu ya kubishania bei. Wenzenu wanaolima korosho, wameacha kukopa na bei mnazisikia kila mwaka zinapanda,” amesema.

“Ukiwa na mazao yako utaweza kubishana na mnunuzi. Tanzania bei ya tumbaku iko chini sababu wakulima mmetufikisha hapo kwa kupitia mikopo na mikataba na makampuni ya ununuzi. Kuanzia sasa badilikeni, ili muweze kuinua bei ya zao hili muhimu, alisema.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMATATU, JULAI 16, 2018.

No comments:

Post a Comment

Pages