HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

July 09, 2019

NEMC yatoa ufafanuzi kelele na mitetemo chafuzi

Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Dk. Samuel Gwamaka, akitoa ufafanuzi juu ya kelele na mitetemo chafuzi zinazotoka kwenye kumbi za starehe, baa na nyumba za ibada kwa mujibu wa kanuni na sheria ya mazingira kwenye mkutano na  waandishi wa habari uliofanyika jijini Dar es Salaam. (Na Mpiga Picha Wetu). 


Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
 
BARAZA la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limetoa ufafanuzi  kuhusu kelele na mitetemo chafuzi zinazotoka kwenye kumbi za starehe, baa na nyumba za ibada kwa mujibu wa kanuni na sheria ya mazingira.
 

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana kufuatia upotoshaji wa taarifa hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa NEMC, Dkt. Samuel Gwamaka amesema baraza halina mgogoro wowote na taasisi za kidini wala  wamiliki wa kumbi za starehe na baa zaidi ya kutekelezaji wa sheria ya mazingira  na kanuni zake.

“Kumekuwa na upotoshaji mkubwa wa taarifa ambayo ilitolewa awali na NEMC juu ya udhibiti kelele na mitetemo chafuzi kwa lengo la kulinda mazingira,” alisema na kuongeza kuwa  taarifa iliyotolewa na Baraza tofauti ile iliyosambaa kwenye mitandao ya kijamiii.


Kwa mujibu wa Dkt. Gwamaka , taasisi za dini na wamiliki wa kumbi za starehe na baa ni wadau muhimu wa Baraza na hivyo haina budi kukumbushana pale panakuwa na ukiukwaji wa kanuni na sheria. “Tunafanya kazi kwa karibu sana na wadau mbalimbali wa mazingira zikiwemo taasisi za dini na wamiliki wa kumbi za starehe na baa lakini mambo yanapokuwa kinyume na utaratibu basi ni jukumu letu kutoa ufafanuzi wa namna mambo yanavyotakiwa  kwenda,” alisema Dkt Gwamaka.


Dk. Gwamaka alitaja viwango vya sauti vinavyoruhusiwa kulingana na sheria na kanuni za Baraza hilo kwa mtu au taasisi yoyote inayotaka kuanzisha huduma  za baa, kumbi za starehe na shughuli za kidini katika maeneo ya watu. 


“Sauti hupimwa kwa disibeli ambapo kwa nyakati za mchana kwa watoa huduma za dini haitakiwi kuzidi desibeli 60 na usiku desibeli 40, maeneo ya sokoni isizidi desibeli 75 na usiku desibeli 50 na viwandani ni desibeli 85 kwa mchana na 65 kwa usiku ili isiweza kuathiri wakaazi wa eneo husika,” alifafanua.

Aidha Dk. Gwamaka aliwataka wananchi kuomba vibali kwa Mkurugenzi wa Baraza pindi panakuwa na kongamano au mikisha mbalimbali ambapo gharama zake ni shilingi milioni tano na Baraza likijiridhisha litatoa kibali hicho. “Vibali vya makongamano na matamasha hutolewa na Mkugenzi Mkuu wa NEMC na iwapo kibali kitakiukwa basi faini yake ni kati ya milioni tatu na isizidi milioni  saba,” alisema Dkt. Gwamaka na kuongeza
“Siyo lengo la Baraza kumpeleka wananchi mahakamani wala kuwapiga tozo mbalimbali bali  kwa kipindi cha mwezi mmoja tutatoa  elimu juu ya madhara ya kelele hizo na baada ya hapo kanuni zitatumika,” alisema. Dk. Gwamaka alisema kanuni hiyo haitahusu zima moto, magari ya wagonjwa, azana misikitini pamoja na kengele za makanisani. 


NEMC kwa siku za karibuni wamekuwa katika  ufanisi mzuri kiutendaji hasa kutokana na mafanikio makubwa waliyoyapatikana kutokana na katazo la mifuko ya plastiki ambalo liliungwa mkono na wadau wa ndani na nje ya nchi.

1 comment:

  1. Hakika kelele zimezidi mno hasa Baa zinazouza pombe. Mfano niishiko Kagondo Muleba, baa iiywayo Wallet barabara kuu kuelekea Biharamulo,kuna kero. Msaada wa ukaguzi unahitajika. Asante

    ReplyDelete

Pages