December 08, 2020

TFS KUPANDA MITI MILIONI 1 MIAKA 59 YA UHURU

NA SULEIMAN MSUYA

KATIKA kuadhimisha miaka 59 ya Uhuru Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kesho unatarajia kupanda zaidi ya miti milioni 1 katika maeneo mbalimbali nchini.

Hayo yamesemwa Kamishna Mhifadhi wa TFS, Profesa Dosantos Silayo wakati akizungumza na mwandishi wa habari hii.

"Kesho kwenye maneo mengi ya wananchi na maeneo ya wazi tutapanda miti kwa kuwa ndio njia ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na uharibifu wa mazingira.

Mashambani tunaendelea na upandaji ambapo mwaka huu tunapanda miche milioni 22 ya miti mingi jamii ya misindano yaani Pines, Misaji, Mikaratusi, Cedrela, Mkongo, Cyprus na mingine," amesema.

Prof.Silayo amewataka wananchi kujitokeza kupanda miti kwa kuwa ni muhimu kwa mazingira.

Amesema wanapanda miti kwa malengo mbalimbali kama kurejesha uoto mahali ulipopotea, kuhimiza watu kutunza miti na misitu, kubadili mitizamo ya watu kuhusu misitu na miti yaani watu wajue miti hulelewa na hivyo waheshimu hasa ile ya asili.

"Tunapendezesha mandhari ya nchi ambapo katika miji tunaleta dhana pana ya misitu ya mijini ambayo ni muhimu kwenye kupambana na uchafuzi wa hewa," amesisitiza.

Aidha, amesema wanahimiza upandaji wa miti ya jamii mbalimbali hususani ya matunda ili kutoa msukumo wa kuitunza.

Amesema upandaji miti husaidia kupata mazao ya miti toka vyanzo vyetu na kupunguza kutegemea misitu ya asili. 

"Angalia kama kule kwa wachaga wanachanganya kwenye kahawa na kupata majani ya mifugo, kuni na kivuli,"amesema.

Kamishna ametoa wito kwa wananchi na taasisi zenye maeneo ya wazi zipande miti na kuitunza ili kukabiliana na uchafuzi wa hewa na mabadiliko ya tabianchi.

"Upotevu kwa takwimu rasmi ni hekta 372,000 kwa mwaka. Sababu ni nyingi. Ila chache ni 
kilimo hususani cha kuhama hama kinachangia takribani asilimia 70 ya upotevu.

Maendeleo ya miji, miundombinu kama ujenzi wa barabara, nishati ya kuni na mkaa nchi inategemea karibu asilimia 92 ya nishati ya kupikia toka kwenye mimea," amesema.

Pia sababa nyingine ni matukio ya moto, mifugo kwenye misitu, uvunaji haramu japo wamepunguza kwa sasa.

Aidha, amesema mabadiliko ya tabianchi pia huchangia ufanisi mdogo wa misitu au ukame unaopelekea moto.

Pia ukosefu wa matumizi bora ya ardhi kwenye vijii kunasabisha migogoro uvamizi wa misitu kwa makazi, kilomo cha kuhama hama, motopori
na utegemezi mkubwa wa nishati.

"Uelewa mdogo wa wananchi kuhusu faida za misitu watu kupanda miti bila kuitunza, mifugo kula miti iliyopandwa,
miche inakufa na mimea vamizi kwenye misitu nayo shida," amesema.

Ametaja mikoa yote ya Kanda ya Ziwa imeathika zaidi kutokana na maeneo mengi mifugo ilizidi viwango na wafugaji hawapendi kuchunga sehemu zenye miti wakihofia mbungo.

Amesema wafuagaji wengi ukanda huo wanachanganya mifugo na kilimo jambo ambalo linaongeza uharibifu wa mazingira.

"Mikoa ya kati mwa nchi kama Dodoma, Singida Shinyanga hali ya hewa haikuwezesha misitu minene lakini tunaendelea kuhimiza upandaji wa miti inayohimili," amesema.

Kamishna amesema katika kukabiliana na uharibifu wa misitu wanashirikiana na wadau binafsi kama Asasi za Kiraia (NGOs,), makampuni makubwa yaliyowekeza nchini kwa ajili ya kilimo cha miti, taasisi za serikali kama Magereza, Jeshi kwa kuwapa mbegu na vifaa vya bustani wanasaidia kukuza miche wanayoigawa bure maeneo mbalimabli.

No comments:

Post a Comment

Pages