Baadhi ya wafanyakazi wa Ofisi ya Waziri Mkuu na Taasisi wakimsikiliza Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Watu wenye Ulemavu Jenista Mhagama.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Uratibu, Bunge, Kazi, Ajira,Vijana na Watu wenye Ulemavu Jenista Mhagama akizungumza na waandishi wa habari wakati akifungua kikao cha wafanyakazi wa Ofisi ya Waziri Mkuu na Taasisi.
Na Asha Mwakyonde, Dodoma
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Uratibu, Bunge,Kazi, Ajira,Vijana na Watu wenye Ulemavu Jenista Mhagama amewaagiza Makatibu Wakuu wa Ofisi hiyo kuendelea kutoa elimu ya UVIKO-19 kwa wafanyakazi wao.
Kauli hiyo ameitoa jana Januari 5, 2022 jijini Dodoma wakati akifungua kikao cha wafanyakazi wa Ofisi ya Waziri Mkuu na Taasisi zake Mhagama amesema ulimwenguni kote wanahangaika namna ya kujikinga na UVIKO-19.
Amesema ni vema Makatibu hao wakatoa elimu kwa watumishi wa serikali kupata chanjo ya UVIKO-19 lengo likiwa ni kujikinga na maambukizi ya virusi hivyo.
"Naamini tunanza mwaka mpya wa kalenda wa 2022 tunaelekea nusu ya bajeti majukumu ni mengi tuliyofanikiwa na ni mengi tuliyoyatekeleza," amesema Mhagama.
Ameongeza kuwa majukumu yaliyo mbele yao ni makubwa wamalize mwaka wa bajeti wakiwa na mafanikio makubwa hivyo leo (jana),wamefanya kazi kubwa ya kuelimisha juu ya ugonjwa wa Corona.
Waziri huyo amesema kuwa Makatibu Wakuu waendelee kusisitiza suala la kuchukua tahadhari dhidi ya magonjwa ya Corona.
Mhagama ameeleza kuwa ujumbe huo kamati ya kitaalamu iliagiza kila wizara watoe elimu kwa wafanyakazi, wakumbushane kuhusu tahadhari ya kujikinga na UVIKO-19.
"Jambo hili nitalichukua na kulifikisha kwa mawaziri wenzangu kusudi kila wizara ifanye hivi na tutekeleze mikazo hii ya serikali, mafunzo haya ya Covid19 yametusaidia," amesema.
Waziri huyo wa Nchi amefafanua kuwa taarifa alizozipata kwa wale ambao hawajabahatika kupata mafunzo na kuchanja baada ya mafunzo hayo wameenda kupata chanjo.
Amesema jambo hilo la msingi lisiishie kwa wafanyakazi hao hata wakitoka katika mafunzo hayo waendelee kuchukua tahadhari.
Kwa upande wa Mratibu wa huduma za chanjo wa jiji la Dodoma Victor Kweka ambaye amemwakilisha Mganga Mkuu wa jiji hilo Best Magoma amesema serikali imetumia nguvu kubwa kutoa elimu kwa Umma kwa ajili ya kujikinga na ugonjwa wa wa UVIKO-19 pamoja na chanjo na vyombo vya habari mbalimbali vimekuwa vikiongelea namna ya kujikinga na ugonjwa huo.
"Tanzania kama ilivyo nchi nwingine ulimwenguni ilikubwa na ugonjwa wa UVIKO-19 lakini tumekuwa na njia mbalimbali za kujikinga na wanasayansi walienda mbele zaidi kwa kutafuta njia za kuweza kujikinga wakagundua chanjo ya UVIKO-19," amesema.
Mratibu huyo ameongeza kuwa chanjo hiyo ilifanyiwa majaribio kama ilivyo kwa chanjo nyingne na dawa ambavyo zinafanyiwa ikathibitika ni salama na inafaa kwa matumizi.

No comments:
Post a Comment