October 26, 2022

TAMKO LA PAMOJA LA ASASI ZA KIRAIA KUHUSU MAZINGIRA NA TATHMINI YA SHERIA MBALIMBALI ZINAZOONGOZA ASASI ZA KIRAIA NCHINI

 

Ndugu waandishi wa Habari;

 

Asasi za kiraia zimekuwa na mchango mkubwa kwa Taifa, mathalani kwa nafasi zao zimekuwa zikiisaidia serikali na jamii katika kutatua changamoto mbalimbali miongoni mwao zikiwa ni changamoto ya elimu kwa umma, huduma za kijamii, ajira, msaada wa kisheria na nyingine nyingi kwa kuzingatia malengo ya kila asasi kwa nafasi yake. Kwa mfano katika ripoti ya wizara ya afya inayohusu mchango wa mashirika katika kuleta maendeleo ya mwaka 2020 inaonesha kuwa AZAKI ziliweza kuingiza kwenye uchumi TZS 1,423,238,932,193 ambapo kati ya fedha hizo kiasi cha TZS 1,193,502,074,491 kilitumiwa na AZAKI katika kutekeleza miradi mbalimbali kwenye jamii. Pia ripoti hiyo inaonyesha kuwa AZAKI 804 ziliajiri wafanyakazi 8,918 ambapo 6,194 ni watanzania na hivyo kupunguza ombwe la ukosefu wa ajira nchini. Hali kadhalika dodoso fupi iliyofanywa na asasi ya Reach Out Tanzania kwa AZAKI 32 imedhihirisha zaidi mchango wa AZAKI katika kuleta maendelo ya kijamii na kiuchumi.

 

 

Pamoja na mchango mkubwa wa asasi za kiraia bado asasi za kiraia zimekuwa zikikutana na changamoto nyingi katika utekelezaji wa majukumu yao. Miongoni mwa changamoto hizo ni pamoja na kuminywa kwa nafasi ya asasi hizi kutekeleza majukumu yao kwa uhuru, kuwepo kwa sheria nyingi kandamizi zinazolenga kuzibana na kuminya asasi za kiraia, mifumo mibovu ya kiserikali, sera mbovu na hata ukosefu wa vibali wakati wa kutekeleza miradi yao mbalimbali kwa jamii.

 

 

Baada ya maumivu ya muda mrefu kwa miaka ya karibuni sisi kama sehemu ya asasi za kiraia tulikutana katika warsha jijini Dar es Salaam, kutathmini kwa kina mchango wa asasi za kiraia kwa taifa, Mazingira ya utendaji kazi pamoja na tathmini ya sera na sheria zinazoongoza asasi za kiraia nchini na hatimaye kuja na mapendekezo kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Asasi za kiraia, jumuiya za kimataifa na vyombo vya habari juu ya namna ya kuboresha mazingizira ya ufanyaji kazi wa asasi za kiraia nchini.

 

 

Kwa kipindi cha takribani miaka sita (6) iliyopita, asasi za kiraia zimepitia changamoto na mazingira magumu ya kiutendaji kutokana na mitazamo ya wanasiasa na watawala, matumizi mabaya ya sheria kandamizi yaliyoambatana na Mabadiliko lukuki ya sheria mbalimbali zinazoongoza asasi na washirika wake. Baadhi ya Sheria zilizotumika na kufanyiwa marekebisho ni Pamoja na;

 

Sheria ya Magazeti ya Mwaka 1976 ambayo ilitumika kuvunja na kukiuka uhuru wa Habari na kupata Taarifa, huku waathirika wakubwa wakiwa ni gazeti la Mwanahalisi, Mwananchi, Mtanzania na Mawio ambalo lilifungiwa moja kwa moja, hawa wote ni washirika wakubwa wa asasi za kiraia.

 


Sheria za Uhujumu uchumi na utakatishaji fedha, hizi pia zimetumika sana kuzitisha asasi za kiraia Pamoja na washirika wake kiasi cha kutokuwa huru kufanya kazi zao kwa kuogopa kushitakiwa kwa makosa ya uhujumu uchumi na utakatishaji fedha kama ilivyoonekana kwa maafisa mbalimbali wa asasi za kiraia walioathirika kwa sheria hizi.

 

 

Sheria ya Mashirika yasiyo ya Kiserikali ya mwaka 2002, ambayo Pamoja na mambo mengine iliweka kikomo cha usajili wa mashirika yasiyo ya kiserikali na utaratibu wa kuhuisha usajili.

 

Sheria zingine ni pamoja na Sheria ya Makampuni ambayo iliyafuta makampuni ya dhamana (Company limited by guarantee) yaliyokuwa yanafanya kazi bila kutengeneza faida, sheria ya Takwimu ambayo kwa kiasi kikubwa imezuia upatikanaji wa Takwimu huru na kuathiri mashirika yanayofanya tafiti. Pamoja na sheria hizo za kitaifa serikali yetu kwa mara ya kwanza, iliondoa itifaki ya Haki muhimu ya Asasi kuishitaki serikali katika Mahakama ya Afrika haswa katika masuala ya Uvunjwaji wa Haki za Binadamu.

 

Tathimini hii tuliyoifanya kwa umoja wetu inaonesha kwamba licha ya mchango mkubwa wa asasi za kiraia, changamoto hizo za kimfumo, kisera na kisheria kwa takribani miaka sita (6) na Zaidi kwa kiwango kikubwa ziliathiri utendaji na ustawi wa asasi za kiraia na washirika wake kiasi cha baadhi ya asasi za kiraia kufungiwa akaunti zao za kibenki, zingine zilifutiwa usajili wao kwa muda, Zingine zilizuiliwa kufanya Warsha na Makongamano ya ndani, kuzuiliwa kwa muungano wa asasi za Kiraia zenye uzoefu wa muda mrefu katika kutoa elimu ya uraia na uangalizi wa uchaguzi mkuu wa mwaka 2020 yaani Tanzania Civil Society Consortium for Election Observation (TACCEO), vitendo hivi na vingine vingi kwa ujumla wake vilikandamiza na vinakandamiza uhuru wa kazi wa asasi za kiraia.

 

WITO.

Kwa ujumla hali hii imefanya asasi za kiraia na washirika wake hapa nchini kuwa na hofu kubwa katika kipindi hiki. Asasi za kiraia na washirika wake kufanya kazi kwa hofu kuliathiri na kunaathiri kwa kiwango kikubwa uhuru wao na utolewaji wa huduma, ufanyaji wa tafiti, upatikanaji wa habari za kiuchunguzi kwa maslahi ya Taifa. Sisi kama asasi za kiraia baada ya tathimini hii tumegundua utendaji wa asasi za kiraia, utafiti na uibuaji wa taarifa za kina zenye maslahi kwa Umma unazidi kupungua kutokana na hofu iliyojengeka miongoni mwa asasi za kiraia pamoja na washirika wake. Katika hatua nyingine sisi kama asasi za kiraia baada ya tathmini ya kina tunatoa wito juu ya mambo yafuatayo;

i.                    Wito kwa Serikali

▪          Serikali irudishe Imani na kutambua mchango wa asasi za kiraia katika maendeleo kwa kuwa pamoja na mambo mengine husaidia kutekeleza mipango ya maendeleo iliyotolewa na serikali.

▪          Kwa kuwa sheria hizi zilirekebishwa na kuletwa kwa hati ya dharura, Serikali ifanye marejeo ya sheria zote zinaoongoza mashirika yasiyo ya kiserikali pamoja


na washirika wake, ikiwa ni pamoja na Sheria ya mashirika yasiyo ya kiserikali, Sheria ya Utekelezaji wa haki za msingi (BRADEA), sheria ya makosa ya mtandao, sheria ya Takwimu, sheria ya Habari, sheria ya haki ya kupata taarifa, sheria ya uhujumu uchumi na utakatishaji fedha na sheria nyingine nyingi ambazo kimsingi zinaathiri asasi za kiraia na utendaji kazi wao.

▪          Kupitia upya na kurudisha Haki muhimu ya Asasi za kiraia na mtu binafsi kuishitaki serikali katika Mahakama ya Afrika haswa katika masuala ya Uvunjwaji wa Haki za Binadamu pale ambapo Mahakama zetu zimeshindwa kutoa haki au kutokuridhika na uamuzi uliotolewa na Mahakama zetu, kama ilivyokuwa awali katika kifungu cha 34(6) cha Mkataba wa Mahakama ya Afrika (Protocol of the African Charter on the Establishment of African Court on Human and People’s Rights).

 

ii.                  Wito kwa vyombo vya Habari

▪          Kuungana pamoja na asasi za kiraia na wanaharakati katika kuzipinga sheria kandamizi kama sheria ya Habari, sheria ya haki ya kupata taarifa, sheria ya takwimu na sheria za makosa ya kimtandao na kanuni za maudhui ya kimtandao ambazo kwa Pamoja zinaathiri utekelezaji wa majukumu yao ya kutoa Habari kwa umma.

 

▪          Vyombo vya Habari nchini viungane kwa Pamoja kuibua na kuzielezea changamoto zao kwa umoja bila kujali tofauti zao

▪          Viongozi, wahariri na watendaji katika vyombo vya Habari wazingatie Zaidi maslahi ya watanzania wanaowafikishia Habari ili kuepuka kuchagua taarifa zipi ziende hewani na zipi zisiende ili mradi tu utoaji wao wa taarifa hauvunji sheria za nchi.

 

iii.                Kwa asasi za kiraia

·         Asasi za kiraia ziendelee kufanya mapitio ya sera na sheria kandamizi ili kushauri serikali juu ya maboresho yanayo hitajika na kufungua kesi mkakati.

·         ziungane kwa pamoja kuendelea kupaza sauti kwa serikali ili serikali itambue na kuweka mifumo na utaratibu mzuri unao ruhusu utendaji kazi wao.

·         Kutoa elimu kwa umma juu ya haki mbalimbali hususani kwa maeneo ya vijijini ili kujenga uelewa na ushiriki wa wananchi katika kudai haki na kuwawajibisha viongozi na kushinikiza maboresho ya sheria kandamizi.

 

iv.                 Kwa Jumuiya za kimataifa

▪          Jumuiya za kimataifa hapa nchini kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo na wanadiplomasia wenye ushirikiano na mahusiano mazuri na


serikali kuendelea kuishauri serikali kuheshimu misingi ya utawala bora, haki za binadamu haswa uhuru wa kukusanyika, uhuru wa kupata taarifa na haki nyingine ambazo ndio msingi wa ushirikishwaji wa wananchi.

 

 

 

 

IMETOLEWA KWENU NA: -

 

1.  Reach Out Tanzania (ROT)

 

2.  Policy and Legal Assistance Organization (PLAO)

 

3.  Tanzania Students Network Program (TSNP)

 

4.  Binti Makini Foundation

 

5.  Her Education Foundation for Self-Reliance

 

6.  Youth Solidarity for Self-Reliance (YS4S)


No comments:

Post a Comment

Pages