HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

August 19, 2018

KERO ZA ARDHI TABORA ZITATATULIWA NA WAZIRI WA ARDHI -MAJALIWA

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi atakwenda katika Halmashauri ya Manispaa ya Tabora ili kutatua kero kubwa za ardhi.

Ameyasema hayo jana jioni (Jumamosi, Agosti 18 ,2018) wakati akizungumza na wananchi wa Manispaa hiyo katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Uwanja wa Chipukizi.

Waziri Mkuu aliyasema hayo baada ya wabunge na wananchi kueleza changamoto kubwa zinazowakabili ikiwe ya migogoro ya ardhi iliyodumu kwa muda mrefu.

“Waziri wa Ardhi atakuja hapa na ramani zake, atakutana na watendaji na kumaliza matatizo yote makubwa ya ardhi na yale madogo madogo yatashughulikiwa na Mkuu wa Wilaya,”.

Katika hatua nyingine,Waziri Mkuu alisema wilaya zote zinatakiwa zihakikishe zinakuwa na shule moja ya kidato cha tano na sita kwenye kila tarafa nchini na Serikali itapeleka walimu.

Alisema uwepo wa shule hizo utaamsha ari ya wanafunzi kusoma kwa bidii, jambo litakaloongeza idadi ya wanaoendelea na masomo ya kidato cha tano na sita.

Kadhalika Waziri Mkuu aliwaagiza watendaji wote kuanzia ngazi ya halmashauri hadi vijiji wawasimamie wanafunzi wa kike na wahakikishe wanamaliza masomo bila ya kukatishwa.

“Huu ni mkakati wa Taifa tunataka watoto wa kike wote walindwe ili waweze kumaliza shule na marufuku kukatisha elimu yao, iwe kwa kuwapa ujauzito au kuwaoa, adhabu yake ni kali,”.

Waziri Mkuu jana jioni alimaliza ziara yake ya kikazi ya siku tatu mkoani Tabora baada ya kuwa amefanya ziara katika wilaya za Igunga, Nzega na Halmashauri ya Manispaa ya Tabora.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMAPILI, AGOSTI 19, 2018.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiteta  na Mwenyekiti wa CCM wa mkoa wa Tabora, Hassan Kasubi katika mkutano wa hadhara aliouhutubia kwenye kiwanja cha Chipukizi katika Manispaa ya Tabora, Agosti 18, 2018.
PMO 0883 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akiteta na Mbunge wa Viti Maalum mkoa wa Tabora, Munde Tambwe katika mkutano wa hadhara aliouhutubia kwenye kiwanja cha chipukizi katika Manispaa ya Tabora.
Wananchi wa Manispaa ya Tabora wakimsikiliza Waziri Mkuuu, Kassim Majaliwa wakati alipohutubia mkutano wa hadhara kwenye kiwanja cha Chipukizi. 
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akisalimiana na Mbunge wa zamani wa Tabora Mjini, Aden Rage baada ya kuhutubia mkutano wa hadhara katika kiwanja cha Chipukizi kwenye Manispaa ya Tabora, Agosti 18, 2018. Katikati ni Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri. 
  Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akimkabidhi Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Tabora, Kamishina Msaidizi wa Polisi, Emmanuel Nley jumla ya shilingi 1,500,000/= kwa ajili ya ujenzi wa dawati la Jinsia katika Mji wa Tabora na ujenzi wa nyumba ya Mkuu wa polisi  katika wilaya ya Igunga.  Makabidhiano ya fedha hizo  zilizotolewa na Mbunge wa Manonga, Seif Khamis Gulamali (kushoto) yalifanyika baada ya Waziri Mkuu kuhutubiua mkutano wa hadhara katika kiwanja cha Chipukizi kwenye Manispaa ya Tabora, Agosti 18, 2018. Wapili kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri na wapili kushotoi ni Mbunge wa Viti Maalum, Munde Tambwe.
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akihutubia mkutano wa hadhara kwenye kiwanja cha Chipukizi katika Manispaa ya Tabora, Agosti 18, 2018. (Picha zote na Ofisi ya Waziri Mkuu)

No comments:

Post a Comment

Pages