HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

September 14, 2018

MIKOA 14 YATEKELEZA KAMPENI YA UPIMAJI VVU

*Wakuu wa Mikoa iliyobakia waagizwa ‘wakaze buti’

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema hadi sasa mikoa 14 imeanza kutekeleza kampeni ya kitaifa ya kupima VVU kwa hiari pamoja na kuanza mapema matumizi ya dawa za kufubaza virusi vya UKIMWI (ARV) kwa wale watakaogundulika kuwa na maambukizo.

Amesema hadi kufikia Septemba 2018, mikoa ya Arusha, Dar es Salaam, Dodoma, Iringa, Kigoma na Manyara imeanza kutekeleza kampuni hiyo. Ameitaja mikoa mingine kuwa ni Mbeya, Mtwara, Mwanza, Njombe, Ruvuma, Shinyanga, Tabora na Tanga.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo (Ijumaa, Septemba 14, 2018) katika hotuba yake aliyoitoa wakati wa kuahirisha Mkutano wa 12 wa Bunge jijini Dodoma. Bunge limeahirishwa hadi Novemba 6, mwaka huu.

Amewataka Wakuu wa Mikoa ambayo bado haijaanza kutekeleza kampeni hiyo waanze mara moja. “Kwa kutambua umuhimu wa kampeni hii, ifikapo Desemba mosi, 2018 wakati wa kilele cha Maadhimisho ya Siku ya UKIMWI Duniani tutafanya tathmini ya utekelezaji kwa mikoa yote nchini. Kwa msingi huo, nisisitize wadau wote wenye mapenzi mema na nchi hii wasaidie katika utekelezaji wa kampeni hiyo.”

Ametumia fursa hiyo kuwapongeza Wakuu wa Mikoa hiyo 14 na akawataka waendelee kuhimiza wananchi waliopo kwenye maeneo yao hasa wanaume wawe tayari kutambua afya zao kuhusu maambukizo ya VVU kupitia kampeni hiyo.

Juni 19, mwaka huu, Waziri Mkuu alizindua kampeni ya kitaifa ya kupima kwa hiari VVU jijini Dodoma ijulikanayo kama “FURAHA YANGU, PIMA, JITAMBUE, ISHI” ambayo imewalenga Watanzania wote kujitokeza kupima na kutambua afya zao hususan wanaume ambao hawajitokezi kwa wingi kupima na kutambua afya zao.

“Wanaume wengi tumekuwa tukiwatumia wenza wetu kutambua kama tumeathirika au la. Tunakaa majumbani tunasubiri tu, ukimuona mwenza wako anarejea kutoka kliniki akiwa mwenye furaha na wewe unajipa matumaini kuwa umesalimika. Sasa wanaume wenzangu tubadilike, tuanze kuchukua hatua za kupima na kutambua afya zetu,” amesisitiza.


Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema Serikali inafanya juhudi za kuhamasisha kampeni hiyo kupitia kwenye Ligi Kuu ya Mpira wa Miguu Tanzania Bara kwa kushirikiana na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).

“Tunafanya hivyo kwa kutambua kuwa Mpira wa Miguu ni mchezo unaoongoza kwa kupendwa duniani na Tanzania. Aidha, kufuatia hatua ya kituo cha matangazo ya televisheni cha AZAM kuamua kuonesha ligi yetu, watu wengi wamepata mwamko wa kutazama na kufuatilia michezo ya Ligi kuu ya Tanzania. Hivyo, tuna uhakika wa kuwafikia wananchi wengi na kuwahamasisha kuchukua hatua za kupima VVU na wale watakaogundulika kuwa na maambukizo waanze mapema matumizi ya ARV.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
S. L. P. 980,
41193 - DODOMA.
IJUMAA, SEPTEMBA 14, 2018.

No comments:

Post a Comment

Pages