HABARI MSETO (HEADER)


 


Breaking

October 23, 2018

VIGOGO WA WETCU WANAKESI YA KUJIBU

NA MWANDISHI WETU, TABORA


Hakimu Mkazi  Mfawidhi wa Mahakama ya Mkoa wa Tabora Chiganga Mashauri amesema kuwa waliokuwa viongozi wa chama Kikuu cha Wakulima wa zao la Tumbaku Kanda ya Magharibi (WETCU) wanayo kesi ya kujibu hivyo wanatakiwa kuleta utetezi wao.


Uamzi huo umetolewa leo na Hakimu Chiganga baada ya kusikiliza mashahidi 16 wa Jamuhuri katika shauri la Uhujumu Uchumi linalowakabili waliokuwa viongozi  wa WETCU.

Akisoma uamzi huo Hakimu Chiganga alisema ushahidi  uliowasilishwa na Jamuhuri  uliokuwa ukiongozwa na Wakili Mwandamizi  Shedrack Kimaro umegusa mashitaka yote matano yanawakabili  washitakiwa.

Watuhumiwa wa shauri hilo la kuhujumu uchumi namba 2/2017 ni Gabriel Mkandala, John Kusaja, Prosper Mbacho, Hamza Kapera, Francis Penta, Msafiri Said na mfanyabiashara Faras Yassin Abbas.

Mashitaka  matano wanayotakiwa kujibu washitakiwa hao ni  kula njama, kughushi, matumizi mabaya ya ofisi, kufanya manunuzi bila kibali na kuisababishia hasara Mamlaka ya serikali makosa ambayo inadaiwa waliyatenda kati ya Juni Mosi hadi Julai  31/2015.

Shitaka la kwanza la kula njama ya kughushi nyaraka  linawakabili Gabriel Mkandala, John Kusanja,  Msafiri Said na mfanyabiashara Faras Yassin Abbas.


Shitaka la kughushi nyaraka linalowakabili Mkandala,  Kusanja, Mbacho, Kapera na mfanyabiashara  Abbas inalodaiwa kuwa  walilitenda  kati ya Tabora na Dar es salaam kwa kutengeneza Kadi ya usajili wa gari namba T 181 VEN aina ya Toyota V8.

Shitaka la tatu la matumizi mabaya ya ofisi linawakabili Gabriel, Kusanja, Mbacho, Kapera, Francis Penta, na Msafiri Said kuwa walinunua gari namba T 181 VEN jambo ambalo lilisababisha hasara kwa chama hicho cha Ushirika.

Shitaka la nne dhidi ya watuhumiwa hao ni kwamba kwa makusudi  na huku wakijua kufanya hivyo ni kosa  walinunua gari aina ya Toyota Land Cruser V8 bila ya kupata kibali kutoka kwa Mrajisi wa Vyama vya Ushirika nchini.

Ilidaiwa katika shitaka la tano kwa watuhumiwa wote saba  ,kwa makusudi walisababisha hasara  ya milioni  109 Chama hicho  kutokana na kununua gari aina ya Toyota Landcruser V8.

Upande wa utetezi ukiwakilishwa na Mawakili Hassan Kilingo na Kanani Chombala umesema kuwa utakuwa na mashahidi wasiopungua 25 pamoja na nyaraka mbali mbali kutoka Mamlaka ya Mapato –TRA na Ofisi za WETCU.

Shauri hilo limeahirishwa hadi Novemba tano mwaka huu litakaopoanza kusikiliza utetezi wa washitakiwa ambao wameomba kusiwe na hailisho tena.

No comments:

Post a Comment

Pages