HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

March 27, 2019

Samata: Nitagawana zawadi na Kapombe

NA JOHN MARWA
 WAKATI wadau na mashabiki mbalimbali wa soka wakimpigania Beki wa Simba, Shomari Kapombe, kunufaika na zawadi zinazotolewa baada ya Timu ya Taifa ‘Taifa Stars’ kufuzu Fainali za Afrika (AFCON), Nahodha Mbwana Samata, naye amekazia.
Baada ya Stars kufuzu kwa kuwafunga Uganda ‘The Cranes’ Jumapili iliyopita mabao 3-0, juzi Rais Dk. John Magufuli, aliwaalika Ikulu jijini Dar es Salaam kula nao chakula cha mchana na kisha kuwapa zawadi ya viwanja jijini Dar es Salaam.
Mara baada ya tukio hilo, wadau na mashabiki mbalimbali walianza kutoa maoni yao ikiwamo kwenye mitandao ya kijamii, wakitaka TFF waangalie pia nyota waliotoa mchango wao katika safari ya Stars kufuzu, huku wakimtaja Kapombe aliyeumia akiwa na timu hiyo kambini Afrika Kusini wakati ikijiandaa kuivaa Lesotho.
Awali kuelekea mechi ya Uganda, pia Mwenyekiti wa Kamati ya Saidia Stars Ishinde, Paul Makonda, alitoa ahadi ya Sh. Milioni 10 kwa kila mchezaji endapo watafanikiwa kufuzu.
Samata, aliandika kwenye ukurasa wake wa twitter, akiiomba TFF kumjumuisha beki huyo katika zawadi zilizotolewa, kwani anaamini kama Kapombe angekuwa yupo fiti angekuwepo sehemu ya kikosi kilicholiletea Taifa heshima kubwa.
Amesema kama TFF watashindwa kufanya hivyo, anawaomba wachezaji wenzake kumchangia kidogo kidogo na endapo itashindikana, basi binafsi atagawana naye nusu kwa nusu ahadi ya Mwenyekiti wa Kamati ya Saidia Stars Ishinde, Paul Makonda ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam.
“Kama Captain ningeomba TFF imuangalie Shomari Kapombe katika zawadi ambazo wachezaji watapata, ikishindikana basi ningeomba wachezaji wote tumchangie kidogo kidogo na endapo vyote visipowezekana kabisa, basi katika ahadi ya Mh. Paul Makonda, nitagawana nae nusu kwa nusu,” ameandika Samata.
Hata hivyo, Mwenyekiti huyo wa kamati hiyo, hakubainisha ahadi itatekelezwa lini.

No comments:

Post a Comment

Pages