HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

March 26, 2019

TIMU YA TAIFA YA NYIKA KUAGWA MACHI 27

TIMU ya Taifa ya Mbio za Nyika inatarajiwa kuagwa rasmi kesho Machi 27 jijini Dar es Salaam tayari kwa safari ya kwenda mjini Aarhs Denmark katika mashindano ya Dunia 'IAAF World Cross Country' yatakayorindima Machi 30 mwaka huu.

Timu hiyo ya Taifa ambayo ilikuwa kambini jijini Arusha kwa takribani mwezi mmoja chini ya ufadhili wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA), na DStv, iliwasili jijini Dar es Salaam jana tayari kwa safari leo usiku.

Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Shirikisho la Riadha Tanzania (RT), Wilhelm Gidabuday, timu iko katika hali nzuri na vijana wana ari ya kwenda kupeperusha vena Bendera ya Taifa huko Denmark.

Gidabuday, alisema Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Harrison Mwakyembe, ataongoza hafla ya kuipa Baraka za mwisho timu hiyo ikiwamo kukabidhi Bendera ya Taifa, akiungana na viongozi mbalimbali kuanzia saa 8 mchana kwenye ukumbi wa Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Katibu huyo, alisema katika hafla hiyo pia wamemualika Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk. Hamis Kigwangalla, Mwenyekiti wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Mhifadhi Mkuu wa Mamlaka ya Ngorongoro, Mkurugenzi wa Multchoice Tanzania na Kurugenzi za Michezo Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT).
Msafara wa timu hiyo ya Tanzania unaundwa na watu 20, wachezaji 16 na viongozi wanne.

Aliwataja viongozi hao ni Makamu wa Pili wa Rais- Ufundi RT, Dk. Hamad Ndee ambaye ni Mkuu wa Msafara, Kocha Mkuu Meta Petro, Kocha Msaidizi Madai Jambau na Matron Marcelina Gwandu.

Wachezaji kwa upande wa wanaume ni Marko Monko, Joseph Panga ‘Mti Mkavu’, Faraja Damas, Emmanuel Giniki, Gabriel Geay, Francis Damiano na Yohana Elisante.
Wanawake ni Failuna Matanga, Magdalena Shauri, Angelina Tsere, Sisilia Ginoka, Mayselina Mbua, Amina Mgoo, Anastazia Dolomongo, Aisha Magelani na Natalia Elisante.
Timu hiyo itaondoka usiku wa Machi 27 kwa ndege ya KLM na inatarajiwa kurejea nchini Machi 31.

No comments:

Post a Comment

Pages