HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

April 07, 2019

Klabu 10 kuwania ubingwa wa taifa wa kuogelea

Na Mwandishi Wetu
Dar es Salaam. Jumla ya klabu 10 zimethibitisha kushindana katika mashindano ya klabu bingwa ya mchezo wa kuogelea yaliyopangwa kufanyika kwenye bwawa la kuogelea la Shule ya Kimataifa ya Tanganyika (IST), Upanga jijini Dar es Salaam.
Mashindano hayo yamepangwa kufanyika Aprili 13 na 14 na yamedhaminiwa na kampuni za Asas, Samsung, DTB Bank, Snow Cream, Knight Support na kituo cha utangazaji cha Clouds FM.
Mwenyekiti wa Kamati ya maandalizi wa Chama Cha Kuogelea Tanzania (TSA), Hadija Shebe amezitaja klabu hiyo kuwa ni Bluefins, Champion Rise, Mis Piranhas, klabu ya kuogelea ya Mwanza (MSC), FK Blue na Wahoo ya Zanzibar.
Hadija amezitaja klabu nyingine kuwa ni ISM-Moshi, ISM-Arusha,FK Blue Marlins, Talis-IST na mabingwa watetezi, Dar es Salaam Swim Club (DSC).
Alisema kuwa mashindano hayo yamepangwa kuanza saa 2.00 asubuhi siku ya Jumamosi na waogeleaji watashindana katika staili tano ambazo ni Freestyle, Breaststroke, Butterfly, Backstroke na Individual Medley.
Kwa mujibu wa Hadija, waogeleaji hao pia watashindana katika relay katika mashindano ambayo yamepitishwa na Shirikisho la Mchezo wa kuogelea Duniani (Fina) kuwa ya kutafuta alama za kufuzu mashindano ya Dunia yaliyopangwa kufanyika nchini Korea mwezi  Julai.
“Tunatarajia kuona ushindania mkali  kwa waogeleaji wetu ili kutafuta nafasi ya kufuzu mashindano ya dunia. Waogeleaji wengi wapo katika maandalizi ya mwisho mwisho kwa ajili ya mashindano hayo, bado tunahitaji wadhamini wa mashindano haya,” alisema Hadija.
Kwa mujibu wa Hadija, kutakuwa na jumla ya vipengele  vya mashindano 108 na kila klabu imetakiwa kuwakilishwa na waogeleaji wawili katika kila kipengele cha mashindano ambavyo pia vimepangwa kutokana na umri.
“Zaidi ya waogeleaji 200 watashiriki katika mashindano haya makubwa ya Tanzania. Tunaomba wadau wajitokeze kusaidia na kuwapa hamasa waogeleaji wetu ambao kwa sasa wamepata mafanikio makubwa katika mashindano mbalimbali ya kimataifa,” alisema.

No comments:

Post a Comment

Pages