HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

June 27, 2019

WANAUME WATAJWA KUONGOZA KWA KUFANYA VITENDO VYA UKATILI

Mwakilishi wa Katibu Mkuu Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ambaye ni Kamishna wa Ustawi wa Jamii Dkt. Naftali Ng’ondi akizungumza na viongozi wa dini wakati wa kikao baina ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto katika kikao cha kuwajengea uwezo viongozi hao kuhusu Ajenda  ya  Kitaifa ya Wajibu wa  Wazazi /Walezi wa Malezi na Matunzo ya Familia kilichofanyika ukumbi wa Ofisi ndogo ya Wizara jijini Dar es Salaam. (Picha na Kitengo cha Mawasiliano WAMJW).

Na Mwandishi Wetu Dar es Salaam

Jinsi ya kiume imetajwa kuwa ni moja kati ya watendaji wakubwa wa vitendo vingi vya ukatili dhidi ya Mwanamke na Mtoto katika jamii ambavyo vimekuwa vikiathiri malezi ya watoto na ustawi wa familia.
Hayo yamebainika leo jijini Dar es Salaam katika kikao katika ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto na Viongozi wa dini katika kujengewa uelewa kuhusu Ajenda  ya  Kitaifa ya Wajibu wa  Wazazi /Walezi wa Malezi na Matunzo ya Familia.
Akizungumza katika kikao hicho kwa niaba ya Katibu Mkuu Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. John Jingu, Kamishna wa Ustawi wa Jamii Dkt. Naftali Ng’ondi amesema kuwa kwa mujibu wa Utafiti wa hali ya ukatili dhidi ya watoto uliofanyika na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa kushirikiana na UNICEF wa mwaka 2011 unaonesha kuwa mtoto 1 kati ya watoto 3 wa kike na 1 kati ya 7 wa kiume walifanyiwa vitendo vya ukatili kabla ya kufikisha umri wa miaka 18.
Dkt. Ng’ondi ameongeza kuwa asilimia 72 ya wasichana na asilimia 71 ya wavulana walifanyiwa ukatili wa kimwili na vilevile robo ya watoto walifanyiwa ukatili wa kiakili.
“Uandaji wa Ajenda hii umetokana na hali halisi ya ongezeko la changamoto zinazomkabili mtoto hasa zinzaoanzia katika ngazi ya familia” alisema
Kamishna Ng’ondi ameeleza kuwa vitendo vya ukatili pia vimekuwa vikisababishwa na ongezeko la migogoro ya ndoa ambapo imesababisha watoto kukosa malezi ya wazazi wote wawili ambapo amesema kwa mwaka kwa mujibu wa takwimu za Ofisi ya Ustawi wa Jamii inaonesha kwa muda wa miezi tisa kuanzia Julai, 2018 hadi Marchi 2019 jumla ya mashauri ya ndoa 16,832 ukilinganisha na mashauri 13,382 kwa mwaka 2017/2018.
Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Idara ya Manendeleo ya Mtoto kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Bi. Mwajuma Magwiza ameeleza kuwa jamii ya kitanzania inakumbwa na changamoto nyingi zikiwemo ukatili dhidi ya wanawake na watoto na Serikali imekuwa ikiandaa mikakati mbalimbali katika kukabiliana na changamoto hzio ikiwemo Ajenda ya Kitaifa ya Wajibu wa Wazazi/Walezi katika malezi na matunzo ya familia.
Naye Mwakilishi wa Baraza Kuu la Waislam Tanzania (BAKWATA) Sheikh Hassan Said Chizenga amesema kuwa Ajenga hii inatakiwa kushirikisha Sekta nyingine kama vile utamaduni na michezo ili iweke misingi bora katika kujenga maadili ya watoto wetu katika malezi na makuzi yao.
Naye Mkurugenzi wa Huduma za Jamii kutoka Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC) John Riziki amesema kuwa Baraza hilo limejidhatiti katika kuhakikisha wanasaidia na wazazi/walezi katika malezi kwa kufanya somo la dini kufundishwa katika shule za Msingi na Sekondari ili kuhakikisha watoto wanakuwa katika maadili mema.
Kikao hiki cha kuwajengea uelewa viongozi wa dini kuhusu Ajenda  ya  Kitaifa ya Wajibu wa  Wazazi /Walezi wa Malezi na Matunzo ya Familia ambayo kinakuja mara baada ya kuzinduliwa rasmi na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu(Mb) katika Maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika yaliyofanyika mkoani Geita Juni, 16.

No comments:

Post a Comment

Pages