HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

February 26, 2020

Wataalam wa nishati SADC wakutana Dar

NA GOODLUCK HONGO
WATAALAM na Makamishna wa Masuala ya Nishati kutoka nchi 12 za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) wamekutana jijini Dar es Salaam kujadiliana namna na nchi hizo kupata nishati toshelevu hasa vijijini.
Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Zena Saidi, wakati akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam.
Alisema mkutano huo ni sehemu ya mwendelezo wa vikao vya SADC nchini, unahusisha wataalam, wakurugenzi, makamishna kutoka nchi 12 ya jumuiya hiyo ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa uamuzi uliopitishwa na viongozi wa jumuiya hiyo.
Saidi alisema wataalam hao watajadiliana kuhusu uanzishaji wa kituo cha umahiri cha kuendeleza nishati na matumizi bora ya nishati, matumizi ya gesi asili kwa nchi za SADC.
 “Tanzania inatengeza Mradi wa Kuzalisha Umeme wa Nyerere (NHPP), pindi utakapokamilika tunaweza kuuza umeme wa ziada katika nchi za SADC. Tunataka bei ya umeme ipungue, matumizi ya mkaa yapungue  na uhifadhi wa mazingira uboreshwe,” alisema Saidi.
Alisema upatikanaji wa umeme katika nchi za SADC hususani vijijini upo chini ya asilimia tano, hivyo kuna haja ya kuongeza upatikanaji wa umeme katika maeneo hayo.
Kwa upande wake Kamishna wa Nishati na Gesi wa Wizara ya Nishati Tanzania, Adam Zuber alisema wataalam hao pia watajadiliana masuala ya nyuklia, kufanya mapitio, kujadiliana utekelezaji wa miradi mbalimbali kama vile uanzishaji wa kituo cha umahiri cha kuendeleza nishati jadidifu na matumizi bora ya nishati kwa nchi za SADC.
“Kamati ya Nishati ya SADC, wamekutana ikiwa ni utekelezaji wa maamuzi ya marais, ambapo nchi wanachama 12 zimehudhuria, na kituo hicho kitaanzishwa baada ya kupata uhalali wa wanachama 11 kati ya 16 wa jumuiya hiyo, kwa sasa ni nchi nane ambazo zimeshasaini uannzishwaji wa kituo hicho,” alisema Zuber.
Mkurugenzi wa Miundombinu wa SADC, Mapolao Makoena alisema mojawapo ya agenda itakayojadiliwa kwa undani ni mabadiliko ya protokali ya nishati, kwamba maamuzi yake yatapelekwa kwa mawaziri ambao nao watayawasilisha kwa marais wa nchi.

No comments:

Post a Comment

Pages