HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

August 20, 2013

SAHRINGON yazifunda Asasi za Kiraia Tanzania

Na Salum Mkandemba

MRATIBU Taifa wa Mtandao wa Mashirika ya Haki za Binadamu Kusini mwa Afrika (SAHRINGON Tanzania), Martina Kabisama, amezitaka Asasi za Kiraia nchini kusaidia Watanzania katika mchakato wa Katiba unaoendelea ili kuepuka matakwa ya wanasiasa kugubika mchakato huo.

Martina alitoa wito huo jana jijini Dar es Salaam, alipokuwa akichangia mada katika Mkutano wa Asasi za Kiraia za Afrika Mashariki (EACSO), ulioratibiwa na Chama cha Mashirika Yasiyo ya Kiserikali Tanzania (TANGO), kujadili mambo kadhaa, ikiwamo Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Aliongeza kuwa, katika Mkutano Mkuu wa Global Social World wa mwaka 2011, pamoja na mambo mengi, Afrika ilishauriwa kuwa na Asasi za Kiraia zinazoshiriki kwa mapana kuwasaidia wananchi katika michakato ya katiba na sio kukurupukia matakwa ya watawala wa nchi.

“Asasi za Kiraia Tanzania zinapaswa kujifunza kutoka kwa asasi kama hizo za Kenya katika kuwezesha upatikanaji wa katiba inayomtambua na kumthamini Mtanzania masikini, sio kuegemea katika malumbano ya kujadili hatima ya Muungano na kusahau mambo muhimu,” alisema Martina.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Jukwaa la Dira Afrika Mashariki (Vision East Africa Forum), Dk Azaveli Lwaitama, alizitaka Asasi za Kiraia nchini kutohofia tofauti ya kiuchumi baina ya nchini za Jumuiya ya Afrika Mashariki, kwani zina nafasi sawa katika kunyanyua maendeleo ya nchi hizo.

Dk Lwaitama alibainisha kuwa, moja ya changamoto inayoikabili Jumuiya ya Afrika Mashariki ni tofauti ya kiuchumi baina ya mataifa na watu wake, ambayo imo hata miongoni mwa wananchi wa nchi moja, hivyo Asasi za Kiraia zinapaswa kuwaongoza Watanzania kujifunza kutoka kwa wenzao.

“Tofauti ya kiuchumi ipo, lakini Watanzania hatupaswi kuihofia, badala yake Asasi za Kiraia zisimame katika kufanikisha kuwapo kwa mchakato wa Katiba ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, ili kuwawezesha Wanajumuiya kunufaika ipasavyo,” alisisitiza Dk Lwaitama.
Aliongeza kuwa, Katiba ya Jumuiya hiyo, itasaidia uharaka wa maendeleo kwa nchi wanachama, kupitia uwekezaji wa pamoja utakaofanikisha kurejea kwa Mamlaka za Usafiri Majini, Sarafu ya Pamoja na Mashirika ya Reli na Ndege ya Afrika Mashariki.

No comments:

Post a Comment

Pages