HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

May 23, 2016

WAZIRI MKUU KUHUDHURIA MKUTANO WA ADB ZAMBIA

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa anaondoka nchini leo (Jumatatu, Mei 23, 2016) kwenda Lusaka, Zambia kuhudhuria Mkutano wa 51 wa Mwaka wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (51st Annual Meeting of the Board of Governors of the African Development Bank - AfDB) utakaofanyika kesho (Jumanne, Mei  24, 2016).

Waziri Mkuu anahudhuria mkutano huo kwa niaba ya Mheshimiwa Rais, Dk. John Pombe Magufuli.

Mkutano huo ambao utafunguliwa na Rais wa Zambia, Edgar Lungu utajadili masuala ya Nishati na Mabadiliko ya TabiaNchi. Pia utahudhuriwa na Marais Idriss Deby wa Chad, Paul Kagame wa Rwanda na Uhuru Kenyatta wa Kenya. Nigeria itawakilishwa na Makamu wake wa Rais, Yemi Osinbajo huku Msumbiji ikiwazilishwa na Waziri wake Mkuu, Carlos Agostinho do Rosário.

Watu maarufu waliothibitisha kuhudhuria mkutano huo ni pamoja na Kofi Annan, Ashish Thakkar, John Kufuor, Mary Robinson, Mo Ibrahim, Nancy Lee, Ngozi Okonjo-Iweala na Tony Elumelu.

Mkutano huo utakaofanyika kwenye kituo cha mikutano cha kimataifa cha Mulungushi (Mulungushi International Conference Centre) utahudhuriwa na washiriki zaidi ya 5,000 kutoka nchi  54 ambao ni wanachama wa benki hiyo, washiriki kutoka nchi 26 ambazo si za bara la Afrika (non-regional member countries), wawakilishi wa mashirika ya kimataifa, wadau wa maendeleo na wawakilishi wa asasi za kiraia. Wengine ni Mawaziri wa fedha, biashara na uchumi na wataalamu kutoka vyuo vikuu.

Waziri Mkuu amefuatana na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Asantu Kijaji, wachumi kadhaa pamoja na wataalamu wa sekta ya fedha.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
2 MTAA WA MAGOGONI,
S.  L. P. 3021,
11410 DAR ES SALAAM.
JUMATATU, MEI 23, 2016.

No comments:

Post a Comment

Pages