HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

July 02, 2016

Serengeti Boys 'mwendo mdundo',Yaifumua Shelisheli 6-0, sasa kuivaa Afrika Kusini

Kikosi cha Serengeti Boys.

Na Mwandishi Wetu

KIKOSI cha timu ya taifa ya vijana chini ya miaka 17 ya Tanzania 'Serengeti Boys' imetinga raundi ya pili ya michuano ya kuwania kufuzu fainali za Mataifa Afrika (2017 AFCON U-17), baada ya kuwachapa Shelisheli kwa mabao 6-0.

Kwa ushindi huo, Serengeti Boys inayonolewa na Bakari Shime 'Mchawi Mweusi', imefuzu raundi ya pili ya michuano hiyo, ambako itaumana na Afrika Kusini, baada ya kuing'oa Shelisheli kwa ushindi wa jumla wa mabao 9-0, hii ni baada ya kushinda mechi ya kwanza kwa 3-0.

Serengeti Boys ililianza pambano hilo kwenye Uwanja wa Stade de Linate mjini Victoria kwa usongo na iliwachukua dakika tisa tu kupata bao la kwanza, lililowekwa kimiani na Ibrahim Abdallah, kabla ya Mohammed Abdallah naye kuwapatia bao la pili dakika ya 43.

Hadi filimbi ya mapumziko ya pambano hilo ya mwamuzi Ahmad Imtehaz Heeralall wa Mauritius, Serengeti ilikuwa mbele kwa mabao hayo, huku wakitawala mchezo na kuwafunika kabisa wenyeji hao ambao walitangulia kubezwa na vyombo vya habari vya kwao.

Katika kipindi cha pili, Serengeti Boys waliendelea kutawala mchezo na kufanikiwa kupata bao la tatu lililofungwa na Asad Juma Ali katika dakika ya 50 kwa mkwaju wa adhabu ndogo 'free kick' iliyopigwa kiufundi na kuzika rasmi matumaini ya wenyeji hao.

Serengeti Boys iliendelea kuwashambulia Shelisheli na kufanikiwa kupata mabao matatu, hivyo kumaliza dakika 90 kwa ushindi wa kishindo na kufuzu raundi ya pili ya michuano hiyo, ambako inaenda kuumana na Afrika Kusini.

Kwa mujibu wa ratiba ya michuano hii ya kuwania kufuzu fainali za nchini Madagascar, Serengeti Boys itaanza kwa kuifuata Afrika Kusini kati ya Agosti 5 na 7, kabla ya kurudiana jijini Dar es Salaam kati ya Agosti 19 na 21 na mshindi wa jumla kufuzu raundi ya tatu.

Fainali hizo za 11 za Afrika kwa vijana, zinatarajia kufanyika mwakani nchini Madagascar zikihusisha nchi nane, ambazo zinatarajia kufanyika kuanzia Aprili 2 hadi 16 mwakani, zikihusisha wachezaji waliozaliwa kuanzia Januari Mosi, 2000.

Katika mechi ya jana, kikosi cha Serengeti kilipangwa hivi: Ramadhani Kabwili, Israel Mwenda, Nickson Kibabage, Enrick Nkosi, Ally Msengi, Ally Ng'anzi, Mohammed Abdallah, Shaaban Zubeir, Ibrahim Abdallah, Rashidi Chambo na Asad Juma.

No comments:

Post a Comment

Pages