HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

May 21, 2019

TIRA kumwaga tuzo za umahiri kwa kampuni za bima, watumishi

.Zitatolewa Siku ya Maadhimisho ya Bima Sept. 27
.Wasomi na wataalamu 8 waunda jopo la majaji   

NA DEODATUS MKUCHU

KAMISHNA Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Shughuli za Bima (TIRA), Dk. Baghayo Saqware amesema mamlaka hiyo haitasita kuzifungia kampuni za bima zinazokiuka sheria kwa kufanya udanganyifu na kutoa huduma chini ya kiwango.

Dk. Saqware ametoa kauli hiyo leo jijini Dar es Salaam wakati wa uzindua wa tuzo za umahiri katika sekta ya Bima katika kutambua kampuni za bima na bidhaa zake pamoja na juhudi za watu binafsi waliosaidia kutoa mchango wa ukuzaji wa sekta hiyo nchini.

Alisema sekta ya bima nchini inawajibu mkubwa katika kukuza, kuendeleza na kuondoa umaskini wa kiuchumi kwa taasisi na watu binafsi hivyo ni muhimu zikafanya kazi zake kwa kuzingatia sheria. 

"Sekta imara ya bima husaidia na kuvutia wawekezaji kufanya biashara bila hofu hivyo kuendeleza uchumi, sekta hii pia ina mchango mkubwa katika kuendeleza viwanda na kutekeleza kwa vitendo kauli mbinu ya serikali ya awamu ya tano ya kuendeleza viwanda na uchumi nchini, " alisema. 

Kuhusu tuzo, Dk. Saqware alisema tuzo hizo  zitazotolewa kwa mara ya kwanza tangu kuanzishwa kwa Mamlaka hiyo, pia zimelenga kuzitambulisha shughuli za bima kwa wananchi ambao wengi wao bado haijawa na uelewa wa kutosha kuhusiana na masuala ya bima.

Alisema tuzo hizo zenye lengo la kuendeleza weledi wa taaluma ya bima na soko la bima kwa kubainisha, kuthamini, kutambua mchango wa kampuni hizo pamoja na bidhaa zilizofanya vizuri katika soko, zitasaidia uhimarishaji na ukuaji wa sekta hiyo katika kuendeleza shughuli za kiuchumi na kijamii kwa wananchi.

Aidha, alisema tuzo zinazowaniwa katika mchakato huo kuwa ni pamoja na tuzo ya umahiri katika elimu, itakayotolewa kwa kampuni inayotoa elimu kwa umma yenye tija na tuzo ya umahiri katika utoaji wa huduma itakayotolewa kwa kampuni inayotoa misaada kwa wananchi katika sekta ya afya.

Nyingine ni pamoja na tuzo ya umahiri kwa kijana anayeibukia (18-30) itakayotolewa kwa vijana waliotoa mchango katika sekta ya bima kwa jamii katika nyanja ya aujasiriamali, na utafiti unaohusisha urahisi wa upatikanaji wa huduma za bima.

Dk. Saqware aliitaja tuzo nyingine kuwa ni tuzo kwa kampuni bora ya mwaka, itakayotolewa kwa kampuni bora miongoni mwa kampuni za bina nchini.

Tuzo nyingine ni ya umahiri katika bidhaa bora na yenye ubunifu inayotolewa kwa kampuni inayotoa bidhaa iliyobuniwa vizuri na kumnufahisha mwananchi hususani wa vijijini na yenye gharama nafuu.

Aidha, alisema mchakato wa tuzo hizo utakaohusisha majaji nane unatarajiwa kuanza Juni 28 Mwaka huu kwa washiriki kutuma maombi kabla ya kufanyika kwa mchakato wa wananchi kuwapigia kura washiriki unaotarajiwa kufanyika katika ya Septemba Mosi hadi 21 Mwaka huu.

Majaji waliokabidhiwa jukumu hilo zito, ni Peter Ilomo (Mwenyekiti), Rajab Kakosa (Makamu), Dk. Jamal Katundu (Katibu), Oktavian Mshiu, John Ulanga, Neema Kiure Msusa, Sanjay Rughani na Louis Accaro. 

Alisema washindi watakaopatikana chini ya jopo hilo lililosheheni wataalamu na wazoefu wa fani mbalimbali, watatangazwa na kupewa tuzo zao siku ya maadhimisho ya Siku ya Bima nchini yatakayofanyika Septemba 27, jijini Mwanza.

Alizitaja zawadi zitakazotolewa kwa washiriki bora katika vigezo 11, ni pamoja na vikombe na vyeti kwa lengo la kupanua wigo wa upatikanaji wa huduma za bima nchini kuelekea uchumi wa Kati.


Aidha, ni kuhakikisha sekta ya bima inaendeshwa kwa weredi wa hali ya juu kuondoa matapeli waliovamia na kuchafua taswira ya huduma hiyo muhimu kwa maendeleo ya nchi na watu wake.

Kwa upande wa maadhimisho ya Siku ya Bima, ni mara ya tatu kufanyika nchini ambapo katika miaka miwili iliyopita 2017 na 2018, yalifanyika jijijini Tanga.
Katibu wa Taasisi ya Bima Tanzania, Ernest Kilumbi, akizungumza kabla ya kumkaribisha rais wa taasisi hiyo, Bosco Bugali, kutoa hotuba yake wakati wa hafla ya Uzinduzi wa Tuzo za Umahiri wa Kampuni za Bima uliofanyika leo jijini Dar es Salaam.  (Picha na John Dande)
Rais wa Taasisi ya Bima Tanzania, Bosco Bugali (katikati), akizungumza wakati wa hafla ya Uzinduzi wa Tuzo za Umahiri wa Kampuni za Bima uliofanyika leo jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Katibu wa Taasisi ya Bima Tanzania, Ernest Kilumbi na kulia ni Kamishna wa Bima nchini, Dk. Barghayo Saqware.
Kamishna wa Bima nchini, Dk. Barghayo Saqware, akizungumza wakati wa hafla ya Uzinduzi wa Tuzo za Umahiri wa Kampuni za Bima uliofanyika leo jijini Dar es Salaam. 
 Baadhi ya majaji watakaosimamia mchakato wa tuzo hizo.
 Baadhi ya waandishi wa habari wakichukua taswira.
Picha ya pamoja.

No comments:

Post a Comment

Pages