HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

June 10, 2019

MAOFISA WAOMBA USM KUTENGEWA BAJETI

Mkurugenzi Msaidizi wa Shirika la Kuhifadhi Misitu ya Asili Tanzania (TFCG), Emmanuel Lyimo, akizungumza na maofisa misitu, maliasili, kilimo, ardhi, sheria na maendeleo ya jamii kutoka wilaya 16 baada ya kufanya ziara ya siku tatu kujifunza kuhusu Mradi wa Kuleta Mageuzi katika Sekta ya Mkaa Tanzania (TTCS), maarufu 'Mkaa Endelevu' unaotelekezwa katika wilaya Kilosa, Mvomero, Morogoro mkoani Morogoro. (Picha na Suleiman Msuya).

 
Na Suleiman Msuya

MAOFISA misitu, maliasili, ardhi, kilimo, maendeleo ya jamii kutoka wilaya 16 nchini wameiomba Serikali kuandaa muongozo ambao utaelekeza halmashauri kutenga bajeti kwa ajili ya usimamizi misitu ya vijiji kuwa endelevu.

Maofisa hao wametoa ombi hilo baada ya kumaliza ziara ya siku tatu iliyoandaliwa na Mradi wa Kuleta Mageuzi katika Sekta ya Mkaa Tanzania (TTCS) maarufu 'Mkaa Endelevu'iliyofanyika katika vijiji vya Matuli na Mlilingwa wilayani Morogoro mkoani Morogoro.

Mradi wa TTCS unatekelezwa katika vijiji 30 vya wilaya za Kilosa, Mvomero na Morogoro chini ya usimamizi wa Shirika la Kuhifadhi Misitu ya Asili Tanzania (TFCG), Mtandao wa Jamii wa Usimamizi wa Misitu Tanzania (Mjumita), Shirika la Kuendeleza Nishati Asili (TaTEDO) chini ya ufadhili wa Shirika la Maendeleo la Uswis (SDC).

Akizungumza baada ya kumaliza ziara hiyo Ofisa Ardhi na Maliasili wa Wilaya ya Liwale, Damas Mumwi alisema iwapo kutakuwa na maagizo kutoka juu kuhusu uwekezaji wa misitu ni dhahiri uendelevu utakuwepo.

Mumwi alisema iwapo misitu ya vijiji na maliasili zitaangaliwa na halmashauri pekee kuwa uwezekano wa kumalizika.

"Tumeona maendeleo yaliyopatikana kupitia Usimamizi wa Shirikishi wa Misitu (USM) kwenye vijiji hivi nashauri kama Serikali kupitia wizara husika inatoa muongozo kwa halmashauri kutenga bajeti ya USM kama ilivyofanya kwa vijana, wakina mama na walemavu," alisema.

Ofisa Ardhi na Maliasili huyo alisema misitu ni rasilimali muhimu katika kuchochea maendeleo ila kinachokosekana ni uwekezaji kama TTCS ilivyofanya Morogoro.

Kaimu Ofisa Ardhi na Maliasili wa Wilaya ya Mvomero, Sadoyeka Kyaruzi alisema uwekezaji katika sekta hiyo utasaidia Serikali kuweza kutatua changamoto za wanavijiji.

Kyaruzi alisema katika wilaya yao kuna vijiji vitano vilivyopo kwenye mradi ambapo kumekuwa na mabadililo makubwa ya kiuchumi, kijamii na maendeleo.

"Naomba kusisitiza bila kuwepo kwa maelekezo kutoka juu kuhusu utengaji wa bajeti kwa ajili ya USM ni vigumu kupata matoe chanya kwenye sekta hii," alisema.

Kwa upande wake Ofisa Misitu Wilaya ya Tunduru, Paul Onesmo alisema atahakikisha elimu aliyoipata anaipeleka Tunduru ili mradi huo wa mkaa endelevu utekelezwe.

Onesmo alisema iwapo wafanya maamuzi watakuwa na uelewa kuhusu USM ni dhahiri kuwa misitu itakuwa salama na kuchangia maendeleo.

Solomon Benjamin Mkuu wa Idara ya Ardhi na Maliasili Ruangwa alisema wilayani kwao wameshaanza kunufaika na rasilimali misitu hivyo anaamini wakati muafaka wa kusambaza elimu ya mkaa endelevu kwa kushawishi utengaji wa bajeti katika usimamizi wa misitu.

Ofisa Misitu Msaidizi Wilaya ya Songea, Hadija Bakari alisema ziara hiyo imeonesha matokeo chanya kwake hivyo atatumia kila njia kushawishi halmashauri kutenga bajeti katika USM.

Bakari alisema pamoja na ushawishi huo anatarajia kutoa elimu kwa wananchi umuhimu wa utunzaji wa misitu kwa dhana ya endelevu.

Gravas Mwalyonbo Ofisa Misitu Namtumbo alisema mradi huo unapaswa kusambazwa katika wilaya zote zenye misitu ya vijiji kwani unapunguza uvunaji haramu wa rasilimali misitu na maliasili.

Alisema halmashauri zinapaswa kuweka kipaumbele katika sekta ya misitu na maliasili kama ilivyo kwa elimu, afya, miundombinu na kilimo.

Ofisa Maendeleo ya Jamii wilaya ya Morogoro alisema Florence Mwambene alisema mradi huo umesaidia kuondoa changamoto nyingi katika vijiji vilivyo kwenye mradi.

Mwambene alisema katika vijiji vya Mlilingwa, Matuli, Diguzi na Tununguo wa navijiji wameboresha maisha yao kupitia mradi huku uhifadhi ukiimarika.

Meneja Misitu Wakala wa Misitu Tanzania (TFS), Benadetta Kadala alisema kiujumla mradi umeonesha matokeo chanya ila kinachohitajika ni kuwepo kwa mipango endelevu baada ya mradi kuisha.

Ofisa Misitu Mkuu Idara ya Misitu na Nyuki Wizara ya Maliasili na Utalii, Seleboni John alisema yeye kama mtaalam wa misitu ameona manufaa na kuahidi kufikisha kwa wakubwa zake kuangalia nanma ya kusambaza mradi huo.

John aliwataka maofisa hao kuandaa taarifa sahihi kuhusu walichojifunza ili wakurugenzi na wafanya maamuzi katika ngazi zao waweze kusukuma mbele zaidi.

Mkurugenzi Msaidizi wa TFCG, Emmanuel Lyimo alisema msingi mkubwa waliotumia kutekeleza mradi huo ni ushirikiano hivyo kuwaomba maofisa hao waliokuja kujifunza kutumia njia hiyo kabla ya kuingia katika utekelezaji.

No comments:

Post a Comment

Pages