HABARI MSETO (HEADER)


Breaking

July 18, 2019

25 UDSM wahitimu kozi ya Ukocha wa Riadha

 Baadhi ya wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), wakiwa katika picha ya pamoja na walimu wao baada ya kutunukiwa vyeti vya Shirikisho la Riadha Kimataifa (IAAF) Level 1. (Na Mpiga Picha Wetu).

Na Makuburi Ally

CHUO Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), kimewataka viongozi wa Vyama na Mashirikisho ya michezo nchini kushirikiana nacho kwa lengo la kukuza na kuendeleza sekta hiyo hapa nchini.

Wito huo umetolewa jijini Dar es Salaam juzi wakati wa hafla ya kukabidhi vyeti kwa wanafunzi 25 wa UDSM waliohitimu Kozi ya Ukocha wa Riadha Ngazi ya Kwanza inayotambuliwa na Shirikisho la Riadha la Kimataifa (IAAF), ‘IAAF Coach Level 1’, na Mkuu wa Idara ya Michezo na Viungo wa chuo hicho, Dk. Steven Mabagala.

Dk. Mabagala, alisema Riadha wameonesha njia kwa kupata elimu ambayo ni njia ya kufikia mafanikio yatakayoisaidia nchi.

Aidha, aliwataka wahitimu wa kozi hiyo, kuwafundisha watoto mchezo wa riadha na kutoviweka kabatini vyeti hivyo na badala yake wavitumie kwa maslahi ya mchezo huo.

"Kozi mliyoshiriki isiwe mwisho, bali mpanue wigo zaidi ya mliyoyapata katika elimu inayotambulika na IAAF," alisema Dk. Mabagala.

Alipongeza kozi hiyo kwa kueleza kwamba, imetolewa wakati muafaka na kuwataka wahitimu hao kuwafundisha watoto kwa sababu hiyo ni kozi ya kitaaluma zaidi.

Naye Katibu Mkuu wa Shirikisho la Riadha Tanzania (RT), Wilhelm Gidabuday, alisema elimu waliyoipata wanafunzi hao ni sehemu ya historia kwa sababu ya unyeti wake.

Gidabuday, alisema sababu ya kuwa ni ya kihistoria ni kwa sababu Mkufunzi aliyeitoa ni sahihi katika mchezo huo.

"Kozi inayotambuliwa na IAAF imempata mtu sahihi ambaye ni Dk. Hamad Ndee, hakuna mwenye mashaka, lakini tunashangazwa kozi nyingi zinazotolewa huko mitaani ambazo hata sisi RT hatuzijui zinatuchafulia mchezo wetu," alisema Gidabuday.

Aidha, Gidabuday alisema wanafunzi hao wa mwaka wa pili chuoni hapo, wamechagua kujifunza mchezo muhimu ambao ni mama wa michezo yote na kuwataka kuongeza juhudi zaidi michezoni.

Mtendaji huyo, alitumia fursa hiyo kueleza kwamba idadi kubwa ya Watanzania imeelekeza akili zao kwenye mbio ndefu na kuwasahau mashujaa walioiletea nchi heshima katika upande mwingine wa riadha, ambako medali ya kwanza hapa nchini ililetwa na mwanamke ambaye ni Theresia Dismas aliyetwaa medali ya fedha mwaka 1965 katika mashindano ya Afrika yaliyofanyika Congo Brazzaville.

Naye Mkufunzi wa kozi ambaye anatambuliwa na IAAF, Dk. Ndee, alisema hiyo ni kozi ya kwanza na ya aina yake hapa nchini, ambayo imeanzia UDSM na baadaye itahamia mikoani.

Naye mmoja wa washiriki wa kozi hiyo, Said Mohamed,  alisema mafunzo waliyoyapata watayafanyia kazi na kueleza kuwa, sio mwisho wao bali wataendelea mbele zaidi.

No comments:

Post a Comment

Pages